Wednesday, September 19, 2012

Taifa la mafukara milioni 30 na mabilionea 30



Raia Mwema
Toleo la 258
12 Sep 2012
MWALIMU wangu wa nje ya darasa, Profesa Issa Shivji, hugawa Watanzania katika madaraja matatu; walalaHoi, walalaheri na walalahai akiwa na maana kwamba watu wenye kuishi kwenye dimbwi la umasikini, watu wenye ahueni na matajiri. Katika mtandao wa kijamii (twitter) wakati naandika makala hii, mdogo wangu Michael Dalali akaniongezea daraja jipya ‘wakeshahoi’. Hawa wa mwisho nadhani ndio tunasema ‘masikini wa kutupwa’ kwa lugha ya mtaani. Sijapata fursa ya kumuuliza Michael ili afafanue hili daraja jipya. Leo ninatafakari na wasomaji kuhusu madaraja mawili tu, walalahoi (mafukara) na walalahai (matajiri).
Mwezi Juni, 2012 niliandika katika lugha ya Kiingereza (The Bottom 30M, www.zittokabwe.com) kujibu swali la kwa nini Watanzania ni masikini licha ya utajiri mkubwa uliopo nchini. Katika makala hiyo ‘Mafukara 30M’ nilihitimisha kwamba Watanzania ni masikini kwa sababu watawala wetu wameamua hivyo kwa kutunga na kutekeleza sera na mikakati ambayo inanufaisha watu wachache katika tabaka la juu la maisha ambao wengi wanaishi mijini na kuacha watu wengi wanaoishi vijijini wakiwa masikini zaidi. Katika tafakuri ya leo nafafanua zaidi huu mtazamo. Watawala wetu ninaamini wakiulizwa tena na wanahabari kwa nini Tanzania ni masikini hawatajibu hawajui (Rais Kikwete na Waziri Mkuu Pinda wamenukuliwa zaidi ya mara moja wakisema hawajui kwa nini nchi wanayoongoza ni masikini). Nimesema na kuandika mara kadhaa sababu za umasikini kuongezeka nchini licha ya kwamba uchumi unaonekana kukua kwa kasi.
Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa wiki iliyopita amerudia tunayoyasema kila siku kwamba ukuaji wa uchumi Tanzania haujapunguza umasikini. Tumekuwa tukisema kwamba mikakati ya kiuchumi tunayotekeleza haimsaidii Mtanzania wa kawaida maana hatuoni tofauti ya maisha yake. Serikali ikaendelea na inaendelea kutekeleza mikakati ile ile ikitegemea kupata matokeo tofauti.
Dk. Mgimwa, Waziri wa Fedha, anasema, “takwimu zinaonyesha kuwa katika kipindi cha miaka 10 iliyopita uchumi umekua kwa wastani wa asilimia saba lakini umasikini umepungua kwa asilimia 2.1 tu ambayo ni ndogo ikilinganishwa na asilimia ya ukuaji wa uchumi”. Akanukuliwa akisema “umasikini umepungua kwa asilimia 2.1 kutoka asilimia 35.6 mwaka 2001 hadi kufikia asilimia 33.4 mwishoni mwa mwaka jana katika kundi la masikini,”. Hakuna kauli mpya hata moja. Kinachosikitisha ni kwamba serikali imeendelea kuona Mpango wa Kupunguza Umasikini na Kukuza Uchumi (MKUKUTA) ndio mkakati pekee wa kuondoa umasikini nchini. Sera na mikakati ya serikali kuondoa umasikini imeshindwa. Taarifa ya Shirika la SID ya mwaka 2012 imeonyesha kuwa kati ya mwaka 2001 na 2011 Watanzania takribani milioni tano zaidi wameingia katika dimbwi la umasikini. Kwa nini uchumi unakua kwa kasi kubwa lakini ukuaji huu haupunguzi umasikini, unazalisha masikini zaidi? Taarifa za serikali pia zinaonyesha kuwa ukuaji wa uchumi hautengenezi ajira kwa watu. Kwa nini hali hii? Kama kawaida hatukosi majibu ya maswali haya. Tunayarudia majibu haya kila wakati tunapopata nafasi ya kueleza. Kwamba sekta za uchumi zinazokua hazina uhusiano wenye nguvu na wananchi wa kawaida – madini, utalii na mawasiliano. Sekta yenye uhusiano mkubwa na wananchi – sekta ya kilimo -  haikui kwa kiwango kinachoweza kupunguza umasikini. Ili kupunguza umasikini Tanzania kwa kiwango kikubwa, sekta ya kilimo inapaswa kukua kwa asilimia zaidi ya nane angalau kwa miaka mitatu mfululizo na kuendelea kukua kwa wastani wa asilimia sita kwa miaka 10.
Jibu lipo na limeshasemwa sana lakini jawabu halisemwi. Labda tuulize tena. Kwa nini sasa sekta ya kilimo haikui kwa kiwango kinachotakiwa ili kuondoa umasikini Tanzania? Jawabu langu ni kwamba watawala hawataki. Watawala wetu wamechagua Watanzania wengi wabakie mafukara. Umasikini wa Watanzania ni chaguo mahususi la watawala kwa kuamua kutekeleza sera ambazo zinakuza kipato cha mwenye nacho na kufukarisha wananchi wengi wa vijijini. Vile vile uamuzi wa watawala kushindwa kupambana na ufisadi na ubadhirifu wa rasilimali za umma ni kitendo cha kumzubaisha katika ufukara mwananchi wa vijijini ambaye anakoseshwa huduma za jamii na miundombinu ya kumpa fursa ya kufaidika na shughuli zake za kiuchumi. Ufukara wa mamilioni ya Watanzania ni matokeo ya chaguo la watawala kisera, kimkakati na kimatendo.
Ufukara ni tofauti na umasikini ingawa tunatumia maneno haya tukiamini kuwa yana maana inayofanana. Wakati umasikini (poverty) ni hali ya kukosa huduma za msingi kama elimu, afya, chakula, maji safi na salama kunakotokana na kukosa kipato au kuwa na kipato kidogo, ufukara (impoverishment) ni hali ya kukoseshwa huduma za msingi za kibinadamu  hata kama kuna juhudi za dhati za kufanya kazi kwa bidii ili kupata uwezo wa kufikia huduma hizo. Umasikini unaweza kusababishwa na masuala mbalimbali ikiwemo hali ya kuwa masikini tu (‘we are poor because we are poor’) au jiografia na mengineyo. Ufukara unatokana na kufukarishwa. Unatokana na uamuzi wa kisera katika taifa husika (au mataifa ya nje) ambayo yananyonya juhudi za watu kupata maisha yenye kuwapa huduma zote za msingi kama elimu, afya, maji na muhimu zaidi chakula cha uhakika. Mafukara wote ni masikini, ila masikini wote sio mafukara. Nitafafanua.
Mwaka 1991 Watanzania masikini wanaoishi Dar es Salaam walikuwa ni takribani asilimia 28.1 ya wakazi wote wa Jiji. Miaka 16 baadaye, asilimia 16 ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam walikuwa wanaishi kwenye umasikini. Kwa upande wa Watanzania wanaoishi vijijini, mwaka 1991 kulikuwa na masikini asilimia 40 ya wakazi wote wa Tanzania vijijini. Mwaka 2007, miaka 16 baadaye, asilimia 37 ya Watanzania wa vijijini walikuwa wanaishi kwenye dimbwi la umasikini. Takwimu hizi unazipata kutoka Ofisi ya Takwimu na Shirika la Twaweza limerahisisha taarifa hizi kupitia chapisho lao “Growth in Tanzania: Is it reducing poverty?”
Masikini wanaoishi Dar es Salaam na miji mingine nchini wanaweza kujikwamua kutoka umasikini kutokana na fursa zinazojitokeza mijini. Miundombinu ya usafiri na usafirishaji, viwanda vipya na fursa za ajira zinajengwa zaidi mijini kuliko vijijini. Huduma za elimu na afya zinaboreka zaidi mijini na hata walimu na manesi wanakimbilia kufanya kazi mijini ambako wamerundikana kuliko vijijini ambako kuna upungufu wa kutisha wa wafanyakazi wa sekta hizo. Masikini wa mijini sio mafukara.
Masikini wanaoishi vijijini licha ya kufanya kazi kwa bidii na hasa kazi za kilimo hawana fursa za kuondokana na umasikini. Mfumo wa uchumi wa nchi umejengwa kwa misingi kwamba watu wa vijijini hupokea bei za kuuza mazao yao kutoka mijini na vile vile hupokea bei za kununua bidhaa zinazotengenezwa mijini kutoka huko huko. Barabara za vijijini zina hali mbaya au hazipo kabisa. Huduma za jamii kama elimu, maji na afya ni mbaya. Huduma za nishati ya umeme hazipo kabisa katika vijiji 96 kati ya vijiji 100 nchini. Masikini wa vijijini ni mafukara. Wamefukarishwa kutokana na sera zinazonyonya jasho la kazi yao kwa upande mmoja na sera zinazowanyima maendeleo ya miundombinu kwa upande mwingine. Asilimia 75 ya Watanzania wanaishi vijijini hivi sasa na kwenye ufukara mkubwa sana. Kwa makadirio ya idadi ya watu Tanzania, Watanzania milioni thelathini waishio vijijini ni mafukara.
Kufunguliwa kwa miundombinu ya vijijini kama barabara, maji na nishati ya umeme kunaweza kuwaondoa watu wa vijijini kwenye minyororo ya ufukara kwenda kwenye umasikini na hatimaye kutokomeza kabisa umasikini. Lakini watawala wanaogawa rasilimali ya nchi hawataki. Wanasema hakuna rasilimali fedha za kutosha kusambaza umeme vijijini ili kukuza viwanda vidogo na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, kusambaza maji safi na salama ili kuboresha afya na kumpunguzia mwanamke wa kijijini muda wa kutafuta maji na kujenga barabara za vijijini ili wakulima wafikishe mazao yao sokoni. Ikifika kujenga shule na zahanati na vituo vya afya wananchi wa vijijini wanaambiwa wajenge wenyewe, wajitolee. Ni kweli hakuna fedha za kuwekeza vijijini?
Ufisadi unatengeneza mabilionea
Itakumbukwa kwamba mwaka 2007, Bunge la Tisa liliibua kashfa mbalimbali zinazoonyesha namna ambavyo fedha za nchi zinavyoibwa na viongozi wenzetu wachache. Haina maana kwamba mabunge ya nyuma hayakuwa na wabunge wenye uwezo au ujasiri wa kuibua masuala ya msingi kuhusu fedha za nchi, lakini nadhani wakati au mazingira hayakuwa yanaruhusu. Tulishuhudia ufisadi uliofanywa Benki Kuu ya Tanzania kwa kuibwa kwa zaidi ya shilingi bilioni 133 za Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), utoroshaji mkubwa wa fedha zilizofikia dola za kimarekani milioni 136 kupitia mradi wa Meremeta uliokuwa chini ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), uingiaji wa mkataba wa madini ya dhahabu wa Buzwagi uliokuwa na thamani ya dola za Marekani milioni 400 bila kuzingatia uhitaji wa kuboresha mazingira ya nchi kufaidika na utajiri wa madini na wizi mkubwa wa fedha za msaada wa kuagiza bidhaa kutoka Serikali ya Japani (Commodity Import Support) ambapo zaidi za shilingi bilioni 40 ziligawiwa kwa viongozi kadhaa wa serikali na wafanyabiashara.
Kashfa chache zilijadiliwa sana ikiwamo ile ya mkataba wa kununua umeme wa Richmond ambao sasa unelekea kuliingiza hasara taifa ya zaidi ya shilingi bilioni 90 kutokana na hukumu ya kampuni iliyorithi mkataba wa Richmond dhidi ya Shirika la Umeme (TANESCO), ile ya Buzwagi ambayo ilisababisha kuundwa kwa Kamati ya Bomani na matokeo ya kamati hiyo ni kuandikwa kwa sera mpya ya madini ya mwaka 2009 na Sheria mpya ya Madini ya mwaka 2010 na ile ya EPA iliyosababisha baadhi ya watuhumiwa kufikishwa mahakamani lakini kuacha kitendawili kikubwa kuhusu Kampuni ya KAGODA ambayo ilikwapua zaidi ya shilingi bilioni 40 katika shilingi bilioni 133 zilizoibwa. Masuala ya MEREMETA na Import Support yamezimika na mshawasha wa wafuatiliaji wa mambo kufuatilia masuala haya umepungua sana.
Masuala hayo machache yaliyoibuliwa katika Bunge la Tisa yanaonyesha kwamba kuna rasilimali fedha nyingi katika taifa ambayo ingeweza kutumika kuwekeza kwenye maendeleo ya watu wa vijijini. Hata hivyo, rasilimali fedha hii inatumika kufanya Watanzania wachache kuwa mabilionea kwa njia haramu za kifisadi. Bunge la Kumi, ninaamini, litaibua masuala mengine zaidi yanayoonyesha namna ambavyo tumeamua kuwafukarisha Watanzania wengi na kuwabilionesha wachache.
Matrilioni kutoroshwa kila mwaka
Katika Kitabu cha ‘Africa’s Odious debts: How foreign loans and capital flight bled a continent’ waandishi Leonce Ndikumana na James Boyce wameonyesha kwamba katika kipindi cha miaka 40 jumla ya dola za Marekani bilioni 11.4 zimetoroshwa kutoka Tanzania kwa njia mbalimbali. Hizi ni sawa na wastani wa dola za Marekani milioni 285 kutoroshwa kila mwaka kuanzia mwaka 1970 mpaka 2010. Sehemu kubwa ya fedha hizi zinatoroshwa na kampuni kubwa za kigeni zinazofanya biashara na kuwekeza hapa nchini (utoroshaji mkubwa umefanyika mara baada ya Tanzania kuanza kuzalisha dhahabu kwa wingi na kampuni kubwa za nje kuanza kutafuta mafuta na gesi asilia kwenye pwani ya Tanzania katika Bahari ya Hindi) na sehemu nyingine ni bakshishi wanayopewa maofisa wa serikali wanaofanikisha utoroshaji huu. Watanzania hawa (wanasiasa, watendaji, maofisa wa jeshi na usalama wa taifa na wafanyabiashara) huficha fedha hizi chafu kwenye benki za ughaibuni na hasa Uswisi, Dubai, Mauritius, Afrika ya Kusini na maeneo mengine (Tax Havens/Offshore/Treasure Islands). Wengine wamewekeza kwenye mali zisizoondosheka kama nyumba na zinazoondosheka kama hisa kwenye kampuni mbalimbali duniani.
Taarifa rasmi ya Benki ya Taifa ya Uswisi inaonyesha kuwa Watanzania wameficha huko zaidi ya dola za Marekani milioni 196. Uchunguzi unaoendelea unaonyesha kuwa takribani Watanzania 30 wameficha fedha zao katika benki za Uswisi. Hii ni bila kuhusisha wale ambao wameficha fedha zao kupitia uwekezaji katika ujenzi wa nyumba na hisa kwenye kampuni mbalimbali duniani na hasa katika nchi za Mauritius, Afrika Kusini na Dubai. Uchunguzi pia unaonyesha kuwa Mtanzania mmoja ambaye hana rekodi yeyote ya biashara zaidi ya utumishi wa umma ameficha takribani dola milioni 56 katika benki mojawapo nchini Uswisi. Serikali ya Tanzania mpaka sasa imekataa kuchukua hatua za kuwajua Watanzania hawa na kuhakikisha kuwa mabilioni haya yanarejeshwa nchini na kuelekezwa kwenye miradi ya maendeleo vijijini. Serikali ya Senegal hivi karibuni imetuma maombi rasmi kwa Benki ya Dunia kuisaidia kufanya uchunguzi na kurejesha nchini mwao mabilioni ya fedha yaliyofichwa kwenye benki za nchi za Ulaya na hasa Uswisi.
Ufisadi unafukarisha
Tanzania ina mtandao wa barabara wa zaidi ya kilometa 85,000 zikiwamo za vijijini na wilaya zinazosimamiwa na halmashauri za wilaya na za mikoa pamoja na barabara kuu (zinazosimamiwa na TANROADS). Fedha zinazotoroshwa kila mwaka ni sawa sawa na kutorosha takribani kilometa 800 za barabara za lami kila mwaka kwa kutumia gharama za sasa za ujenzi wa barabara. Fedha hizi pia zinaweza kuunganisha umeme kwenye vijiji 1,300 (asilimia 10 ya vijiji vyote nchini) kila mwaka kwa gharama za sasa za kuunganisha umeme tena kwenye mikoa ambayo haipo kwenye gridi ya taifa (REA wanatumia takribani shilingi bilioni saba kusambaza umeme katika vijiji 16 vya Jimbo la Kigoma Kaskazini). Fedha hizi pia zingeweza kuajiri walimu wengi zaidi wa vijijini na kwa kuwa miundombinu ya umeme, barabara na maji ingekuwa imeboreshwa walimu hawa wangekaa vijijini na kufundisha watoto wetu. Ufisadi kama huu umekosesha nchi rasilimali za kuendeleza watu wake.
Rushwa na ufisadi inatengeneza Watanzania wachache kuwa mabilionea. Mabilionea hawa ambao wana ushawishi mkubwa katika kuunda sera za nchi na utekelezaji wake wanasababisha kuundwa kwa sera na sheria zinazolinda utajiri wa walionacho na kuendelea kuhakikisha masikini wanaendelea kuwa mafukara. Rasilimali za nchi zinaboresha maeneo ambayo mabilionea na wasaidizi wao wanaishi na kusahau kabisa kwamba Watanzania wengi wanaishi vijijini na huko ndipo kuna umasikini mkubwa. Umasikini wa vijijini kwa kiasi kikubwa unatokana na sera na matendo yanayofukarisha wananchi wengi.
Ukuaji wa uchumi unaoambatana na ufisadi wa kiwango kinachotokea Tanzania unawafanya wenye nacho kupata zaidi na masikini kuwa mafukara zaidi. Tofauti ya kipato katika jamii imezidi kuongezeka na inaweza kuleta machafuko katika nchi. Takwimu za Pato la Taifa, kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa 2011, zinaonyesha kwamba asilimia 30 ya Watanzania (the richest 30%) wanamiliki asilimia 75 ya Pato la Taifa.
Tumeona kwamba Watanzania mafukara wanaishi vijijini, asilimia 75 ya Watanzania,  na hivyo takribani Watanzania milioni 30 wanaoishi vijijini wanaishi katika dimbwi la umasikini. Vile vile tumeona kwamba asilimia 30 ya Watanzania wanamiliki asilimia 75 ya Pato lote la Taifa. Pato la Taifa mwaka 2011 lilikuwa shilingi 40 trilioni na hivyo asilimia 30 ya Watanzania wanamiliki shilingi trilioni 30 katika jumla ya shilinig trilioni 40. Kutokana na muundo wa uchumi wetu ambapo sekta ya huduma (service sector) na ile ya viwanda (industrial sector) zinachangia zaidi ya asilimia 70 ya Pato la Taifa na ukweli kwamba sekta zinazokua kwa kasi ni pamoja na mawasiliano, madini, ujenzi na utalii, ni dhahiri Watanzania na kampuni za kitanzania wanaomiliki zaidi ya shilingi trilioni moja hawazidi thelathini na kuna watu wanaweza kuwataja mmoja mmoja kwa majina yao au majina ya kampuni zao.
Kwa hiyo Watanzania milioni thelathini wamefukarishwa kwa kunyimwa fursa za kiuchumi na hivyo kumiliki sehemu ndogo sana ya Pato la Taifa. Wanafanya kazi kwa bidii lakini mfumo wa kinyonyaji unawaweka katika umasikini wa kudumu. Tumeona kuwa uchumi wa nchi unazalisha kundi dogo la watu wenye utajiri mkubwa ambao sehemu kubwa umepatikana kwa njia haramu. Watu hawa pia wanamiliki sekta za uchumi zinazokua kwa kasi na hivyo utajiri wao unazidi kuongezeka. Hawa wanashirikiana na Watanzania walio katikati (walalaheri) kuhakikisha wanaendelea kumiliki uchumi wa nchi. Hawa watu wa kati ndio wanasiasa, warasimu serikalini, wafanyakazi wa kada ya kati ya kampuni za matajiri hawa au zinazofanya biashara na matajiri hawa. Badala ya watu wa kati kuweka sera madhubuti za kumkomboa Mtanzania wa chini aondokane na ufukara, wanaweka mazingira mazuri kwa matajiri kutajirika zaidi. Hatimaye tunajenga Taifa la Watanzania mafukara milioni thelathini na mabilionea thelathini. Tukatae.
Tunaweza kujenga taifa la watu wenye fursa sawa kwa kufanya uamuzi wa kubomoa mfumo wa kiuchumi wa kinyonyaji tulioanza kuujenga tangu tupate uhuru kwa kuacha kubomoa mfumo wa uchumi wa kikoloni licha ya Azimio la Arusha. Juhudi za kujenga taifa lenye watu sawa ziliyeyuka mara baada ya kuamua kufuata sera za ubinafsishaji ambapo zilitafsiriwa kwa kukabidhi mali za taifa kwa kundi dogo la watu na hivyo kutengeneza mfumo wa kifisadi ambao sasa umeota mizizi. Kazi zilizofanywa kwa miaka 20 ya kujenga uchumi wa viwanda ziliyeyushwa katika kipindi cha miaka mitano tu na viwanda vyote viligawanywa kwa watu binafsi na vingi leo ni maghala tu ya kuhifadhi bidhaa nyingine.
Ufisadi mkubwa ulishamiri kupitia sera ya ubinafsishaji ambapo watawala waliokuzwa kwa ‘kanuni’ ya ‘kutosheka’ walijawa na tamaa kubwa na uroho wa mali na kuanza kukusanya chochote kilichokuwa mbele yao. Hivi sasa nafasi yoyote ya uongozi imekuwa ni nafasi ya ulaji na sehemu kubwa ya tabaka la watawala kuanzia kwa wenyeviti wa vijijiji, madiwani, wabunge, mawaziri na hata marais wamekuwa ‘rent seekers’ yaani watu ambao ni lazima kulimbikiza mali kutokana na nafasi za utawala walizo nazo. Mfano wa wabunge kulilia nyongeza ya posho za kukaa kitako wakati walimu na madaktari wanaishi katika mazingira magumu ya kazi ni moja ya tabia za kutotosheka na tamaa zinazopamba viongozi wa kisiasa wa zama hizi.
Kutochukua uamuzi madhubuti wa kutokomeza ufisadi na mfumo wake ni kufukarisha Watanzania kwa sababu rasilimali inayopotea kupitia vitendo vya kifisadi ingeweza kuwekezwa katika maendeleo ya watu wa vijijini, kwa kukuza shughuli za kiuchumi na kupanua mapato ya wananchi. Hivi sasa vita dhidi ya ufisadi imekuwa ni turufu ya kisiasa tu na sio mchakato maalumu wa kuondoa kabisa mfumo wa kifisadi. Ni lazima kuondoka kwenye hali ya kwamba; ushujaa ni kutaja tu fulani na fulani ni fisadi, hali ambayo imefikia hata watu wasio na chembe ya uadilifu kuchafua wengine, na kwenda mbele zaidi kwenye hatua za kubomoa mfumo wa kifisadi.
Hata uchumi ukue kwa kasi ya namna gani iwapo ukuaji huo unanufaisha kikundi kidogo cha watu hauna maana na ni hatari kwa uwapo wa taifa lenyewe. Ni lazima kuchukua uamuzi wa kujenga taasisi zenye nguvu ambazo zitaondoa hali hii ya uchumi kutajirisha wachache na kufukarisha wengi. Taasisi na mfumo utakao hakikisha kuwa watawala wanawajibika kwa umma kwa wanayoyatenda na wasiyoyatenda. Mfumo utakaohakikisha kuwa rasilimali za nchi zinarudi kwa wananchi ili kujenga miundombinu vijijini ya barabara, maji, nishati ya umeme na huduma za kijamii hasa elimu na afya. Vinginevyo tutaendelea kuwa taifa vipande vipande kutokana na tofauti kubwa ya kipato na fursa ndani ya jamii. Tanzania yenye mafukara milioni thelathini na mabilionea thelathini haikubaliki


No comments:

Post a Comment