Saturday, September 8, 2012

Kesho Mungu akipenda nitakuwa ndani ya Sumry kuelekea Bukoba halafu Kampala..


Ndugu zangu,

Mungu akinipa uhai na afya kesho nitakuwa safarini kuelekea Uganda, nafuatilia masuala yangu ya shule mjini Kampala.

Kwa muda mrefu tangu mwaka 2008 nimekuwa nikitumia njia moja tu kuenda na kurudi Kampala njia ya Arusha-Nairobi. Ni mara moja tu nilitumia njia ya Tanga-Mombasa wakati nilipokuwa nikirudi mwanzoni mwa mwaka huu.

Lakini kwa kuwa sasa nina kitu cha kusemea, nataka kutumia njia ya Bukoba nipitie mpaka wa Malaba nitokee Masaka kusini mwa Uganda.

Lengo ni kupata taswira ya nchi yetu maana kwa njia hiyo ya kupitia Bukoba nitafanikiwa kupita mikoa takriban saba ama minane. Niliwahi kupita mpaka wa Malaba mara moja nikielekea Bukoba kutoka Kampala. Ni katika kampeni za uchaguzi wa mwaka 2010-2011 zilizomrudisha madarakani kwa mara nyingine Rais Yoweri Kaguta Museveni. Nilikimbia vurugu za Museveni na Dr Kiiza Bessyige nikarudi nyumbani lakini niliishia Bukoba nikakaa wiki moja halafu nikarudi Kampala, hivyo sikuifaidi mikoa mingine.

Mara hii nitafanikiwa kupita mikoa kuanzia Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma, Singida, Shinyanga, Mwanza na Bukoba. Si mzuri sana wa ramani ya upande huu lakini nadhani mikoa hiyo nimeipatia vizuri kutoka Dar es Salaam kuelekea Bukoba.

Ni safari ndefu na ya kuchosha kidogo, lakini mara nyingi hupenda kuona mikoa mingi zaidi ya nchi yetu kubwa. Kadhalika nitajionea karaha za barabara mbovu na hali halisi ya maisha ya mtanzania alie mikoani.

Tumeshajizoesha kuishi mjini, hatuoni mambo mengi yanayowasibu watu huko mikoani hasa maeneo ya vijiji. Yapo mambo mengi sana wananchi wa vijijini wanataka viongozi wayaone. Miundombinu mibovu, zahanati chache tena zisizo na sifa, vyumba vya madarasa visivyo na hadhi na hata vyenye hadhi havina walimu wa kutosha. Matatizo ya maji na umeme. Yapo mengi sana ambayo nitajionea.

Ningetamani kupata fungu zuri la pesa halafu nikawa nasafiri kwa mafungu mpaka nifike safari yangu, yaani kila mkoa nishuke na kukaa siku moja. Lakini kufanya hivyo kunahitaji pesa ya kutosha na kama mnavyofahamu blogu yenu ni changa haijaanza kupata matangazo. Lakini hiyo ni ahadi naiweka, Mungu anisimamie niweze kuitimiza, ipo siku nikipata ufadhili nitaizunguka Tanzania na kuanika kila tatizo linalokumba watu wa vijijini. Maana magazeti yetu yanaandika habari za mjini tu na za kina Diamond na Mr Blue.

Labda niwape siri, nawapenda sana watu wa vijijini, ningetamani sana siku moja maisha yangu niyahamishie huko nami niwe mkulima. Lakini nikihamia vijijini blogu ya kidojembe itakosa wa kuiendesha maana vijiji vingi vya Tanzania havina huduma ya mtandao, na hata ukiwepo unakuwa chini sana. Ingawa si vijiji vyote.

Mwalimu Nyerere, alipata kutamka kuwa kama tunataka maendeleo ya nchi kwanza tuimarishe vijiji vyetu. Tukipeleka huduma nzuri vijijini kama Zahanati na Hospitali kubwa, kuanzisha mashamba makubwa ya mazao ya biashara na chakula, maduka makubwa ya pembejeo za kilimo, shule za kisasa zenye walimu wa kutosha, barabara inayopitika kwa kipindi chote. Na mambo mengi mazuri.

Basi mjini kutakosa watu, maana watu wote watahamia vijijini kufanya kazi, hii itapunguza msongamano mijini na hata ikibidi baadhi ya ofisi za serikali zikahamia huko vijijini itaamsha ari ya watu kuendeleza vijiji ili pawe mahala bora pa kuishi.

Matokeo yake Tanzania nzima itajengwa na itachochea wawekezaji na hata wageni watakuwa wengi kwa maana watu hupenda maendeleo. Pesa itakuwa na mzunguko mzuri na hata thamani yake itapanda, hivyo uchumi utakuwa kwa haraka bila kutarajia. Wawekezaji hawataki kutuletea maendeleo, wanachotaka ni kuona tunajiendeleza wenyewe ili waje kuwekeza.

Aidha, vijijini ndipo palipo na wapiga kura; watu wa mjini hawana muda wao wanatafuta pesa muda wote. Lakini cha kushangaza viongozi wakishakwenda kuomba kura huko vijijini wanarudi mjini na kusahau kabisa kama kuna watu waliwaahidi jambo. Maendeleo yote huyaleta mjini. Kule mpaka baada ya miaka mitano ndipo wanarudi tena.

Nifupishe mjadala huu kwa kusema nakwenda kuwatazama watanzania halisi. Watanzania wanaoilisha nchi hii na kuendelea kuwaweka madarakani viongozi ambao hawawakumbuki lakini hawakati tamaa kuwapokea kila wanapoona umaarufu wao kisiasa unapungua.

Kesho nitakuwa safarini jembe lenu niombeeni nirudi salama. Sitorudi mikono mitupu nitawaletea zawadi; na zawadi ya mwandishi ni picha na habari..

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
09/09/2012 

<

No comments:

Post a Comment