Saturday, September 1, 2012

Soma habari ya mechi leo Coastal Vs Young African..

Nilichojifunza mchezo wa leo kati ya Coastal Union na Yanga uwanja wa taifa.

Ndugu zangu,

Siku zote husemwa mficha maradhi kifo kitamuumbua, leo nimeshuhudia timu yangu ya Coastal Union ikifungwa goli mbili moja na vijana wa jangwani. Hakuna mtu ambae alishuhudia mechi ile ya leo na kushindwa kuwamwagia sifa vijana wa Coastal.

Hakika walicheza kandanda ya kufurahisha sana na ya kutia hamasa sisi washabiki kutegemea mambo mengi mazuri kwa msimu ujao wa 2012/2013.

Kuanzia dakika ya kwanza mpaka dakika ya thamanini vijana wa Coastal walimiliki mpira, wakatoa pasi za uhakika na chenga zenye kuonekana kiasi mashabiki wa Yanga wakawa kimya kabisa. Hata goli lililofungwa kipindi cha kwanza cha mchezo na Razak Khalfan, lilikuwa la kiufundi na hata namna walivyoweza kuzuia mashambulizi ya Bahanuzi kila mtu alifurahi.

Hata kipindi cha pili kilipoanza bado uhai wa Coastal ulionekana hasa katika upande wa viungo na beki zote za kulia na kushoto ingawa kulikuwa na uhai mdogo katika safu ya umaliziaji lakini inaweza kurekebishika.

Tatizo lilikuwa kwa golikipa wa Coastal Juma Mpongo, bado anaonekana ana wasiwasi na anapangua sana kuliko kudaka mipira. Tatizo hili ni dogo ikiwa kocha wa magolikipa Bakari Shime, atafanya maamuzi ya haraka lakini litakuwa kubwa kama ataendelea namna hii katika ligi kuu.

Tuende katika mada ya msingi, upo upinzani mkubwa katika klabu ya coastal Union iliyo na makazi yake mjini Tanga barabara ya 11. mashabiki asilimia thamanini hawamtaki kocha, naam Juma Mgunda kocha mkuu wa timu hiyo hatakiwi hata kidogo na mashabiki wa wagosi wa kaya.

Na leo nimegundua makosa mengi ya kocha huyo, timu ilikuwa katika nafasi nzuri sana ya kushinda, lakini makosa madogomadogo yaliyotoa upenyo kwa Mbuyu Twite kupiga shuti na mchezaji wa coastal Jamal, kujifunga kwa kichwa wakati akijaribu kuokoa hatari hiyo; yaliwapumbaza wachezaji wa Coastal maana kwa dakika mbili walikosa nguvu hasa baada ya kujiona wapo pungufu baada ya mchezaji mwenzao Jerry Santo kupewa kadi nyekundu kwa kumtukana mwamuzi.

Lakini badala yake Kocha alitakiwa kusimama na kuwaambia wachezaji wasijali kujifunga ama timu pinzani kusawazisha ni moja ya mchezo. Lakini hakufanya hivyo bali aliendelea kukaa katika benchi la wachezaji wa akiba bila kusema lolote. Kazi kubwa alikuwa akifanya kocha msaidizi Habib Kondo, ambae alionekana kusimama muda wote wa mchezo.

Kocha wa timu pinzani hakika alionyesha uwepo wake, hakukaa hata kidogo mbali ya timu yake kuwa nyuma kwa goli moja na kuonekana kuelemewa lakini bado alikuwa akiwapigia kelele wachezaji wake na kuwaita kuzungumza nao kila alipopata nafasi. Hilo sikuliona kwa kocha wetu mchezaji wa zamani wa Coastal Union Juma Mgunda.

Hakujaharibika kitu, lakini ipo haja kukaliwa kikao kwa mashabiki wote nchi nzima kujadili suala hili. Maana nimesikia mashabiki wa Dar es Salaam wanamtaka kocha na mashabiki wa Tanga hawamtaki, kwakuwa mashabiki wa Tanga ndiwo wanaokaa na wachezaji kwa muda mwingi wanaweza kuwashawishi kwa maneno ama kuwarubuni wauze timu ili ionekane kocha hafai. Na hii ni mbaya sana kwa mustakabali wa klabu hasa ikizingatiwa tunaingia katika msimu mpya muda si mrefu.

Rai yangu ni kukaliwa kikao ambacho kitaamua nini cha kufanya maana nimesikia mpaka wiki iliyopita katika mechi ya kirafiki baina ya Polisi Dodoma na Coastal kocha alitaka kupigwa na mashabiki mpaka ikabidi kupewa ulinzi wa polisi.

Hatutafika popote kama tutaendelea na msuso huu, nimeshangaa sana timu imekuja kutoka Tanga bila viongozi wa juu wala kikundi cha ngoma ambacho mara nyingi hujitolea kuja kwa nauli zao….. Tafakari maneno haya mpenzi wa Coastal..

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
1/09/2012













No comments:

Post a Comment