Tuesday, August 28, 2012

leo imetimia miaka 26 tangu kufariki mpambanaji Sheikh Thabit Kombo Jecha (AMMI)

Hapa ni mji mkongwe mjini Zanzibar, Thabit Kombo (alievaa kanzu na koti) akiwa na Rais wa kwanza wa Tanzania Mwalimu Nyerere, pembeni kulia ni Makamu wa kwanza wa Rais Tanzania na Rais wa kwanza wa Zanzibar huru Abeid Karume.


KUMBUKUMBU YA MIAKA 26 YA KIFO CHA SHEIKH THABIT KOMBO JECHA AL-SHIRAZY (AMMI).


Leo mwanamapinduzi maarufu wa Zanzibar na Tanganyika Sheikh Thabit Kombo Jecha Al-shirazy (AMMI) ametimiza mika 26 tangu kuiaga dunia mnamo Tarehe 28 Agosti,1986 kwa maradhi ya Moyo, akiwa na umri wa miaka 82.

Leo kwa wale walioshuhudia msiba huo wanakumbuka simanzi iliyowakuta miaka 26 iliyopita lakini vijana wa umri wetu ambao kipindi hicho hatukujua kilichokuwa ni muda Muafaka kwetu kutafakari na kuyadurusu Maisha ya Mzee wetu Thabit Kombo kwa lengo jema la kujikumbusha, kujifunza na kuchukua yale yaliyo mema kwa ajili ya Mustakali na Maslahi Mema ya Nchi yetu.

Waswahili wa Tanga wana kauli yao Maarufu itokanayo na Laghaja za Kimtang'ata isemayo "Usinene ukamara (usiseme ukamaliza)" ambayo wanadaiwa waliitohoa kwenye Kauli Maarufu ya Sheikh Thabit Kombo ambayo alipenda kuitoa kusisitiza busara ya kufanya maamuzi na subira katika taharuki, Kombo alisema "Weka Akiba". 

Thabit Kombo Jecha Al-shirazy aliekuwa maarufu kwa neno lake ‘weka akiba ya maneno’ alilolipenda kila aliposisitiza jambo la msingi alitunukiwa kipawa kikubwa cha busara, hekima na upambanuzi wa hali ya juu wa mambo. Siku zote yeye alikuwa ni mtu wa kati na kati, akitumika kusuluhisha penye matatizo na kuleta mshikamano pale penye utengano.

Busara yake ya kimatamshi na uchaguzi wake wa maneno kuntu yenye tasfida njema, yasiyokera na yenye kuueleza ukweli mchungu pasi na kukufanya ukereke siku zote vilimtofautisha na wenziwe wengi, maisha yake yote ameshuhudiliwa kama msuluhishi mwema, mleta utulivu katika Jamii yake na mpatanishi muhimu katika hali tete.

Mwaka 1984 wakati aliyekuwa Rais wa Zanzibar na Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bwana Aboud Jumbe Mwinyi akitaka kuvuliwa Madaraka yake yote na Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi Sheikh Thabit Kombo Jecha alikuwa amelazwa Katika Hospitali ya KCMC akitibiwa maradhi ya Moyo.

Kwa kutambua uzito wa jambo lililotaka kufanyika na kutambua athari mbaya ya matokeo yake ikiwa busara na hekima ya hali ya juu haitatumika, ndege Maalum ilitumwa kwenda kumfuata Moshi na kumpeleka Dodoma ili akashiriki Kikao husika.

Sheikh Thabit Kombo Jecha Al-Shirazy alizaliwa Mwaka 1904 Jijini Unguja. Ni miongoni mwa wale wakongwe wachache ambao tunaweza kuthubutu kusema kuwa waliona mengi na walikula chumvi nyingi.

Moja ya Matukio ya kukumbukwa kuhusu maisha ya Sheikh Thabit Kombo Jecha ni vita kati ya Tanganyika na Zanzibar ambavyo vilitokea mwaka 1914 wakati huo yeye akiwa na miaka 10 tu.

Wakati ule wa Vita kuu ya kwanza ya Dunia Mzee Thabit anakumbuka sana Mashambulizi yale ya kupokezana kati ya Meli ya inayoitwa Lord Minna (Ujerumani) kuipiga Meli ya Pegasus (Uingereza) iliyokuwa imepaki kwa ajili ya Matengenezo katika Bandari ya Zanzibar. Baada ya siku tatu za hekaheka Waingereza wakaagiza Manowari (man-of-war) nyingine kutoka India inayoitwa SS Charlton, ikaenda kupiga Dar es Salaam. Charlton ikafanikiwa kuipiga Minna, meli ya Wajerumani, na kuivunja vipande vipande; likavunjwa hata gati la kupandishia meli, Baadaye Charlton ikarejea Zanzibar.

Mara baada ya mashambulizi hayo ya kupokezana kati ya Waingereza na Wajerumani Ikawa vita ndiyo vimekwishaanza kati ya Waingereza na Wajerumani. Ikabidi sasa serikali ya Sultani kufanya utaratibu wa kuwapata raia kwenda vitani "kusaidia" katika ulinzi unaosimamiwa na Waingereza. Hakuwako raia aliyependa kujiandikisha kwenda vitani; wao hawakuwa na sababu ya kupigana vita, na tena kila mtu alikuwa na hofu kwamba akienda vitani atakufa, hana nafasi ya kurudi hai.

Basi mbinu zikafanywa za kuwakamata raia kwenda vitani; na waliokamatwa wakatokea kuwa Wahadimu tu, yaani Waafrika. Waarabu, Wahindi na Wangazija hawakukamatwa. Basi Waafrika wengi wakapata sababu nzuri ya kuhamia kabisa mashambani, wakauhama mji kwa kuogopa kupelekwa vitani.

Baada ya kuwakosa Wahadimu kwa kipindi, Waingereza wakabuni hila nyingine ya kupiga bendi, matarumbeta na ngoma za kienyeji. Bendi ilipigwa na askari wa K.A.R. ambao wengi wao walikuwa wanatoka Kenya; Wakamba, Wajaluo, na kadhalika, watu wa Zanzibar wakawaita askari hao "Mburumburu” (sauti ya matarumbeta). Basi bendi ilipopigwa vijana walifuatia kwa mamia mpaka pwani Malindi. Huko ikawa imeandaliwa meli maalum, na vijana walipofika huko wakachukuliwa kwa urahisi na kupelekwa Tanganyika kujiunga na vita.”

Baada ya Elimu ya awali na kujitambua, Sheikh Thabit Kombo Jecha alizitumia vilivyo nguvu zake katika kufanya kazi, na alikuwa jembe kweli kweli maana hakuchagua kazi. 

Alivua, alifanya Kazi kwenye Shirika la Reli (Maarufu kama Bububu Express), aliuza duka na mwishoni mwa miaka ya 30 alifanya biashara ndogondogo kabla ya kuajiriwa kama Mkuu wa Ulinzi katika Chama cha Wakulima wa Tumbaku (Ambacho kilikuwa kama Shirika la Serikali).

Wakati akiendelea kufanya kazi katika Karakana ya Kuhifadhia Karafuu kama Mkuu wa Ulinzi, Sheikh Thabit Kombo Jecha aliunga Urafiki na baadhi ya Wafanyakazi ambao walikuwa na Elimu kubwa kiasi kuliko yeye, Wafanyakazi hao ni kama Bwana Shab Abeid na Bwana Ajmi Abdallah, ambao walimuingiza kwenye Utungaji wa Mashairi na pia Vyama vya Muziki.

Katika wakati husika Jamii kubwa ya Kizanzibari ilikuwa imegawanyika katika Matabaka Mbalimbali, ya kidini, kikabila na hata asili. Vyama kama Shirazy Association, African Association, Indian Association, Hadhramaut na Oman Association vilikuwa ni mambo ya kawaida tu.

Sheikh Thabit Kombo Jecha kama Wanajamii wengine wa wakati huo naye alijiunga na Chama chao cha Washirazi kilichoitwa Shirazi Association, na Mwaka 1956 alichaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa Chama hicho katika Tawi la Unguja, hatimae akawa katibu mkuu wa chama cha ASP baada ya kuunganishwa African Association na Shirazi Association ikaundwa Afro Shirazi Part (ASP) chini ya uenyekiti wa Abeid Karume .

Na hapo ndipo mlango wa siasa katika maisha yake ulipofunguliwa, alishiriki kila hatua ya kudai uhuru na hatimae mapinduzi ya mwaka 1964. hata baada ya kuunganisha Zanzibar na Tanganyika aliendelea kushika nafasi mbalimbali za juu Serikalini.

Mwaka 1972 wakati Rais wa kwanza wa Zanzibar na makamu wa kwanza wa Tanzania Abein Amani karume kuuwawa kwa kupigwa risasi Thabit kombo alikuwa karibu na Karume hivyo nae kujeruhiwa vibaya kwa risasi kitu kilichomfanya kutembelea magongo mpaka kifo kinamkuta.

Thabit Kombo mpaka anaaga dunia alishika nyadhifa mbalimbali katika baraza la mawaziri Zanzibar na Tanzania. Hii inaonyesha ni namna gani aliaminiwa na marais wote wawili na kumfanya ni mtu wao wa karibu sana wakimtumia kwa ushauri. Hata mwalimu Nyerere alipenda sana kumtumia kwa ushauri mpaka alipokuwa katika kitanda chake cha kifo bado alikuwa akimfuata kumtaka ushauri.

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
28/08/2012

NB: Habari hii nimeiandika kwa kukusanya vipande vya taarifa kila mahali hasa katika ukurasa wa facebook wa bwana Seif Abalhassan ambae ndie alienikumbusha juu ya kumbukumbu hii leo jioni.




No comments:

Post a Comment