Tuesday, August 21, 2012

Someni namna barabara za mabasi yaendayo kasi jijini zitakavyokuwa...


Na Hafidh Kido

Mradi wa mabasi yaendayo kasi jijini Dar es Salaam unategemea kuzalisha ajira elf 80 pindi itakapokamilika awamu ya kwanza ya mradi huo mwaka 2014 ambayo inahusisha barabara ya morogoro kutoka Kimara mpaka Kivukoni.

Akizungumza na kidojembe katika ziara ya kamati ya mradi huo wiki iliyopita mkurugenzi wa mradi injinia Enock Kitandu, alisema mbali na kupunguza msongamano wa magari jijini lakini pia wamelenga kutoa ajira kwa vijana na makampuni binafsi ya kizalendo.

“Hapa kituo cha kivukoni tu tunategemea kutoa ajira elfu 15, na tutakuwa na vituo takriban vine kwa awamu ya kwanza ambapo tunategemea kuzalisha ajira elfu 80, ni hatua kubwa sana hasa kwa kipindi hiki cha matatizo ya ajira. Lakini mbali ya watu watakaoajiriwa lakini kutakuwepo na mambo mengine ambayo yatapasa watu kujiajiri kama kufanya biashara ya vyakula na vinywaji katika vituo na huduma nyingine ambazo hutokea kutokana na mahitaji,” alisema.

Kwa kipindi cha miezi kadhaa kumekuwepo na sintofahamu kwa wakazi wa jijini hasa wale wanaotumia barabara ya morogoro kwa kuona ujenzi unaendelea lakini wengi wao hawakuwa wakijua ni nini hasa kimekusudiwa kujengwa hasa katika kufahamu baada ya ujenzi kukamilika mabasi hayo yataptia wapi, magari madogo yatapitia wapi na waenda kwa miguu watakuwa na nafasi gani.

Kwa mujibu wa injinia Kitandu anaeleza kuwa barabara itakuwa na njia nane, mabasi yaendayo kasi yatakuwa na njia nne za katikati ambazo hazitoingiliana na magari mengine. Halafu njia nne za pembeni (mbili kila upande) zitakuwa za magari madogo ya binafi na waenda kwa miguu watapita pembeni kabisa, ambapo kwa mujibu wa mkurugenzi huyo baada ya ujenzi kukamilika hakutaruhusiwa daladala kupita katika njia hiyo.

Akizungumzia kuhusu aina ya mabasi yatakayotumika alisema kuwa kutakuwa na mabasi ya aina mbili mabasi mlisho; ambayo ni madogo yenye uwezo wa kubeba abiria 60 waliokaa na mabasi makubwa yenye uwezo wa kubeba abiria 140 waliokaa.

“Kutakuwa na mabasi aina mbili mabasi mlisho na mabasi makubwa, haya mabasi mlisho au kwa lugha ya kigeni ‘feeder buses’ kazi yake ni kuchukua abiria kutoka maeneo ya ndani kama kigogo ama magomeni ambamo mabasi makubwa hayapiti na kuwaleta barabarani kupanda mabasi ya kasi.

“Halafu kutakuwa na mabasi makubwa yatakayopewa majina ya Chui, Simba, Duma, Pundamilia, na Twiga kutokana na rangi ambayo yatakuwa na uwezo wa kubeba abiria 140 waliokaa au ikisimamisha; ambapo kisheria inaruhusiwa itakuwa na uwezo wa kuchukua abiria 270 kwa safari moja. Msishangae haya mabasi ni makubwa sana yatakuwa na urefu wa mita 18.5. Na ili kuleta usawa kutakuwa na sehemu ya mizigo na hata viti vya watu wenye mahitaji maalum kama wazee na vilema,” alieleza Kitandu.

Nae mtendaji mkuu wa mradi huo Cosmas Takule, alisema mradi utakuwa na awamu sita lakini awamu ya kwanza itakapokamilika mnamo mwaka 2014 zitakuwa zimetumika kiasi cha Tsh 470bil ambapo pesa hizo zimetoka bank ya dunia. Na kila baada ya miaka miwili watahakikisha wanakamilisha awamu moja hivyo kufanya mpaka kufikia mwaka 2025 jiji la Dar es Salaam litakuwa halina shida ya usafiri kwa namna yoyote ile.

“Hizi fedha Tsh 470bil zinatoka bank ya dunia na ni mkopo usio na masharti, na kila tutakapokamilisha awamu moja watakuwa wanatuletea pesa nyingine kwa ajili ya awamu ya pili. Ambapo awamu ya kwanza itahusisha kilomita 20.9, awamu ya pili 19.3km, awamu ya tatu 23.6km, awamu ya nne 16.1km, awamu ya tano 22.8km na awamu ya sita ni 27.6km.

“Awamu ya kwanza ni barabara za morogoro, kawawa, kivukoni, sokoine na msimbazi. Awamu ya pili itahusisha barabara ya Kawawa upande wa kusini, awamu ya tatu ni barabara ya Nyerere ambapo itapitia mtaa wa uhuru, bibi Titi na mtaa wa Azikiwe. Awamu ya nne barabara ya Kilwa, awamu ya tano barabara ya Mandela na awamu ya sita itakuwa ni barabara ya Old Bagamoyo, nadhani hayo ndiyo maeneo korofi katika msongamano wa magari jijini,” alifafanua Takule.

kidojembe ilipozungumza na kaimu mkurugenzi wa jiji Mussa Matty, ambae ni mjumbe wa kamati ya mradi huo iliyo chini ya uenyekiti wa Meya wa Dar es Salaam Dk Didas Masaburi alisema “Huu mradi umeanzia ofisi za jiji mwaka 2002 ambapo ndipo wazo la kuondoa kero ya msongamano wa magari lilipokuja.

“Mwaka 2010 tulishinda nafasi ya kupata msaada kutoka bank ya dunia ili kutengeneza miundombinu ya barabara za miji mikubwa barani Afika. Kulitangazwa nafasi ya kuandika miradi ili kuweza kuwasilisha bank ya dunia ili kupewa msaada huo, tulishiriki miji mingi lakini baada ya mchujo tukabakia miji mitatu Accra (Ghana), Lusaka (Zambia) na sisi Dar es Salaam.

“Hatimae baada ya mchujo mwingine sisi tukafanikiwa kuibuka kidedea na sasa mnaona mambo yameshaanza. Kamati yetu imetembelea miji mingi kuenda kuangalia maendeleo ya barabara hizi za mabasi yaendayo kasi tumejifunza mengi hasa tulipokuwa Bogota nchini Colombia, naamini tutafanya kile ambacho bank ya dunia ilikusudia kukiona,” Matty.

Hata hivyo mradi wa mabasi yaendayo kasi bado unakumbwa na changamoto nyingi sana kiasi inaweza kuchelewesha mradi kukamilika kwa wakati, kwa mfano mpaka sasa kituo cha gerezani palipokuwa na nyumba za bandari mpaka sasa ujenzi haujaanza kutokana na kesi iliyofunguliwa na wananchi wa eneo hilo kwa madai kuwa hawajalipwa fidia yao.

Mtendaji mkuu wa mradi Cosmas Takule, alisema watu hao walishalipwa pesa zao lakini bado wanasisitiza kupewa zaidi kwa madai kuwa kiasi walichopewa hakilingani na thamani ya ardhi yao kwa wakati huu.

Kwa mujibu wa Takule, gerezani ndiyo itakuwa kituo kikuu cha mabasi hayo lakini mpaka sasa hakuna kilichofanyika hata msingi haujajengwa kutokana na mgogoro huo, maana eneo hilo litajengwa vituo ‘terminal’ vitatu yaani mabasi yaendayo kasi na usafiri wa reli ambao ni mradi mpya wa kukabiliana na msongamano jijini. Pia kutakuwa na jingo la mawasiliano kwa vituo vyote (control centre), ambapo itakuwa ni makao makuu ya mabasi yote kwani taarifa za wasafiri na mwenendo wa mabasi utakuwa unaendeshwa kutoka kituo hicho.

Kuhusu nauli Takule hakutoa majibu ya moja kwa moja juu ya viwango ingawa alisisitiza kuwa mradi huo umedhaminiwa na bank ya dunia bila masharti yoyote maana yake Serikali wala viongozi wa jiji hawatakuwa na maslahi yoyote katika mradi huo ila ni kuhakikisha uendeshaji wake unakuwa mzuri ili kila mmoja aweze kumudu.

“Siwezi kusema nauli itakuwa ni shilingi ngapi lakini nataka kukuahidi kuwa mradi huu umewalenga watu wa hali ya chini, yaani wale wasiokuwa na magari, wasiomudu kupanda bajaji, wasiomudu kupanda daladala tena hasa wale ambao wanatembea kwa miguu.

“Utaratibu utakuwa ni kupewa kadi maalum ambayo utakuwa unajaza pesa kutokana na uwezo wako, ukifika katika vituo vyetu unaingiza katika mashine maalum ambapo utakatwa nauli kutokana na mahali unapokwenda, itakuwa ni gharama ndogo sana. Faida yake ni kuwa kama utajaza pesa katika kazi yako kwa mwezi mzima hata kama huna pesa mfukoni utakuwa unapanda basi kwa mwezi mzima,” alifafanua Takule.

Mji wa Dar es Salaam ni moja ya miji inayokuwa kwa kasi sana katika Afrika hivyo kuvutia watu wengi mbali ya wageni kutoka nchi jirani na nchi za mbali lakini hata watanzania wanaoishi mikoa mingine nchini huvutika na shughuli za kijamii na kiuchumi zinazofanyika Dar es Salaam, hivyo kuufanya ni mji wenye watu wengi kuliko miji yote nchini Tanzania.

Dar es Salaam inakisiwa kuwa na wakazi milioni nne ambapo idadi kubwa ya wakazi asubuhi huenda mjini hivyo kuhitaji usafiri kila siku asubuhi na jioni, hali hiyo huufanya mji wa Dar es Salaam kuwa na msongamano wa magari wakati wa asubuhi na jioni si tu kwa wanaotumia usafiri wa umma lakini hata wanaotumia usafiri wa binafsi adha hiyo inawakumba.

Katika miaka ya nyuma kuliwahi kuja mabasi aina hii yakiitwa ‘icarus’ ambapo yalisaidia sana kupunguza msongamano wa watu katika usafiri wa umma, lakini baada ya kukosa matunzo mabasi yale yalishindwa kuendelea kuwepo barabarani.

Hata hivyo tatizo sasa si idadi ya mabasi yanayotoa huduma bali miundombinu ya barabara kutoandaliwa kuweza kukabiliana na ongezeko kubwa la watu namna hii, hivyo wazo la kutafuta mabasi makubwa yatakayopita njia yake pekee na kutanua barabara kutoka mistari mine mpaka minane inaweza kupunguza adha ya usafiri jijini.

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
21 August, 2012




No comments:

Post a Comment