Sunday, August 26, 2012

Malawi bado haijaacha uchokozi kwa Tanzania....


Na. Aron Msigwa – MAELEZO.

26/8/2012, Lilongwe, MALAWI.

Tanzania imeitaka Malawi kusitisha shughuli za utafiti katika eneo la ziwa Nyasa lenye mgogoro na kusisitiza nia yake ya kuendelea kuzungumza na nchi hiyo kuhusu mgogoro wa mpaka licha ya nchi hiyo kuendelea na msimamo wake wa kumiliki eneo lote la ziwa hilo.

Hayo yamebainishwa katika mkutano wa wataalam na viongozi kutoka serikali ya Malawi na Tanzania kushindwa kufikia muafaka uliokusudiwa kuhusu eneo halali la mpaka unaotenganisha nchi hizo.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha kikao cha usuluhishi kilichohusisha timu za wataalam na viongozi wa wizara husika wa nchi hizo kilichomalizika jana usiku mjini Lilongwe Waziri wa mambo ya nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania Bernard Membe amesema Tanzania bado inaamini katika mazungumzo ili kufikia muafaka wa kudumu wa mgogoro huo.

Amesema kuwa pamoja na sababu mbalimbali zilizotolewa na upande wa serikali ya Malawi juu ya umiliki wa eneo lote la ziwa Nyasa ,msimamo wa Tanzania juu ya mpaka unaozitenganisha nchi hizo uko wazi kwa kwa kuzingatia vielelezo vya historia vilivyoachwa na wakoloni na sheria za kimataifa kuhusu mpaka kuwa katikati ya ziwa hilo.

Ameeleza kuwa licha ya serikali ya Malawi kuonyesha kila dalili za kukwamisha mazungumzo hayo yaliyoanza kupitia vikao mbalimbali nchini humo viongozi wa nchi hizo kupitia mkutano wa kutafuta suluhu uliomalizika jana usiku wameamua kuunda timu za wataalam

“Licha ya kuwasilisha vielelezo kuonyesha uhalali wa mpaka hatukuweza kufikia muafaka tumefika mahali pa kuhitaji msaada tuzitume tume za nchi zetu zitoe mapendekezo ya nini kifanyike maana kuna kila dalili kwamba sisi wenyewe tutashindwa kuendelea zaidi “

Amesema kuwa wataalam kutoka Malawi na Tanzana watakutana mwezi Septemba jijini Dar es salaam ili waweze kutoa mapendekezo ya namna bora ya kuwapata wasuluhishi wa mgogoro huo pamoja na kutoa mapendekezo ya faida na hasara ya njia watakazozipendekeza.

“ Sasa tumefika mahala pa kuhitaji msaada,tutazituma timu zetu zikae pamoja na kutoa mapendekezo ya nini kifanyike maana inaonyesha wazi kabisa sisi wenyewe hatutaweza kuendelea tena sasa timu zitatoa mapendekezo juu ya kesi hii tuwaite wazee wenye busara barani Afrika tunaowaamini watuamulie” amesema.

Amefafanua kuwa timu za wataalamu zitakazoundwa zinatarajia kukutana mwezi Septemba jijini Dar es salaam ili kutoa mapendekezo ambayo yatapelekwa kwa marais wa nchi hizo katika kuelekea hatua ya pili ya utatuzi wa mgogoro huo ikiwemo kumtafuta msuluhishi au kwenda kwenye mahakama ya Kimataifa.

Aidha , Tanzania imeitaka Malawi kusitisha shughuli za utafiti katika eneo la Tanzania katika ziwa Nyasa lililo na mgogoro na kukisisitiza kuwa mchakato wote wa kutafuta suluhu utaendeshwa kwa amani na utulivu huku akiwaomba watanzania kuendelea kuiombea nchi amani ili suala hilo limalizike kwa amani ,utulivu na undugu.

Kwa upande wake waziri wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya kimataifa wa Malawi Bw. Ephraimu Chiume katika maelezo yake wakati wa kuhitimisha mkutano huo amesisitiza kuwa licha ya mgogoro huo kuhitaji busara zaidi bado serikali yake inaamini kuwa mpaka kati yake na Tanzania uko upande wa mashariki mwa ziwa Nyasa na unatenganishwa na ardhi ya Tanzania.

Amesema kutokana na unyeti wa suala lenyewe na eneo hilo pamoja na historia ya nchi yake anapenda kuona ufumbuzi ukipatikana haraka ili wananchi wa nchi mbili waweze kuendelea na shughuli zao bila hofu yoyote.

“Ni matumaini yangu mkutano wa Dar es salaam utaofanyika mwezi Septemba utazaa matunda ili suala hili lipatiwe ufumbuzi na ikiwezekana tupate msaada wa sheria za kimataifa kwa sababu suala hili liko kisheria zaidi” alisisitiza Bw. Chiume.

Ujumbe wa wataalam kutoka Tanzania uliokuwa ukitafuta suluhu ya mgogoro huo uliwahusisha makatibu wakuu Patrick Lutabanzibwa (Ardhi),John Haule(Mambo ya nje) na mawaziri wa wizara ya Ardhi Prof. Anna Tibaijuka na Bernard Membe wa Mambo ya Nje na ushirikiano wa Kimataifa, balozi wa Tanzania nchini Malawi Patrick Tsere pamoja na wataalam wanaotoka eneo la ziwa Nyasa akiwemo Prof.Hemphrey Kamisama ambao nao walitoa maelezo kueleza hisia za wananchi wa eneo hilo na uhalisia wa ziwa hilo.

No comments:

Post a Comment