Friday, July 27, 2012

Sheria mpya za mifuko ya jamii zimewakeraje!!! wananchi?........



MABADIKO ya Sheria ya Hifadhi za Mifuko ya Jamii ya mwaka 2012, iliyopitishwa Aprili mwaka huu, imeendelea kuzua mtafaruku sehemu mbalimbali nchini, huku wabunge wakishinikiza kuwa, sheria hiyo inapaswa kurejeshwa bungeni ili ijadiliwe upya.

Jana, wabunge waliunga na wafanyakazi kupinga kipengele cha sheria hiyo kinachomtaka mfanyakazi kupata mafao yake baada ya kufikisha umri wa kustaafu kwa hiari ambao ni miaka 55, au miaka 60 kwa mujibu wa sheria.

Hoja ya kutaka suala hilo lijadiliwe upya ilitolewa na Mbunge wa Kisarawe (CCM), Selemani Jafo ambaye aliungwa mkono na Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu na Mwenyekiti wa Bunge ambaye pia ni Mbunge wa Peramiho (CCM), Jenista Mhagama.

Hoja ya Jafo ilitokana na kuwapo kwa taarifa kuwa, zaidi ya wafanyakazi 600 katika migodi minane nchini wameacha kazi huku wengine zaidi ya 4,000 wakiwa tayari wamewasilisha barua za kuacha kazi kutokana na sheria hiyo.

Hata hivyo, Mbunge wa Mwibara (CCM), Kangi Lugola alitofautiana na wenzake pale aliposema kuwa sheria inayolalamikiwa ilishapitishwa na Bunge, hivyo angependa kujua uhalali wa kujadiliwa tena bungeni.

Jijini Dar es Salaam, mjadala mzito uliendelea huku baadhi ya wanasheria waliozungumza na gazeti hili wakisema: “Marekebisho hayo ni kandimizi na yanalenga kuwanyima haki wanachama ambao wanaweza kupata matatizo mbalimbali wakiwa kazini”.

Kwa upande wake Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA), jana ilitoa taarifa iliyoweka bayana kuwa, fao la kujitoa kazini limefutwa na kwamba jambo lolote linalohusu mafao ya aina hiyo linapaswa kusubiri kutolewa kwa miongozo husika.

No comments:

Post a Comment