Monday, July 30, 2012

Rais Museven wa Uganda azungumzia Ebola nchini kwake.


Rais wa Uganda Yoweri Museveni amewataka watu kuepuka kugusana moja kwa moja baada ya virusi hatari vya Ebola kuenea katika mji mkuu Kampala.
Watu kumi na wanne wamekufa akiwemo mmoja mjini Kampala, tangu kuzuka kwa ugonjwa huo magharibi mwa Uganda wiki tatu zilizopita, alisema katika taarifa maalum kwa Taifa.
Ebola ni moja ya magonjwa hatari duniani.
Unaenea kwa kugusana na unaua mpaka 90% ya watu walioambukizwa.
Bw Museveni alisema maafisa wa afya wanajaribu kufuatilia kila mmoja ambaye ana waathirika ili kwamba waweze kuwekewa Karantini.
Watu hawana budi kuepuka kuepeana mikono, kubusiana au kufanya mapenzi kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo, aliongeza.
Bw Museveni alisema ndugu na amrafiki wasimzike mtu yeyote anayehisiwa kuwa amekufa kwa Ebola.
"Badala yake awaite wafanyakazi wa afya kwa sababu wanajua namna ya kufanya mazishi hayo,” alisema.
Bw Museveni alisema madaktari saba na wafanyakazi 13 katika hospitali ya Mulago hospitali kuu ya rufaa mjini Kampala – wako kwenye karantini “baada ya tukio la mtu mmoja au wawili” kupelekwa huko.
Mtu mmoja aliyeathirika baadaye alikufa.
"Nawatakia kheri, na Mungu azipumzishe kwa amani roho za wale waliokufa " Bw Museveni alisema wakati akimaliza hotuba yake kwa Taifa.
Muathirika wa kwanza wa ugonjwa huu alikuwa mama mjamzito katika wilaya ya Kibaale kiasi cha kilometa 170(maili 100) magharibi mwa Kampala.
Baadaye ukasambaa wakati wa mazishi, alisema Rais Museveni.
Uganda imekuwa na milipuko mikubwa mitatu ya ugonjwa huu kwa miaka 12 iliyopita.
Uliokuwa hatari kabisa ni wa mwaka 2000 wakati watu 425 waliambukizwa. Zaidi ya nusu yao walikufa.
Hakuna chanjo ya virusi hivyo. Dalili zake ni kupata homa ya ghafla, udhaifu, kuumwa kichwa kutapika na matatizo ya figo.
 Chanzo: BBC Swahili

No comments:

Post a Comment