Friday, May 10, 2013

Je unamjua Sir Alex Ferguson?



Wapenzi wa mpira wa miguu duniani hasa wale wanaoshabikia ligi ya Uingereza jana walishikwa na butwaa baada ya kocha mkuu wa klabu kongwe ya Mnachester United, Sir Alex Ferguson kutangaza kujiuzulu kuifundisha klabu hiyo iliyotangaza ubingwa wa ligi hiyo mapema mwezi huu.
Kwa wale wanaofuatilia maisha ya nguli huyo habari hizi hazijawashitua sana kwa maana kwa kipindi kirefu amekuwa akitajataja kustaafu kuifundisha klabu hiyo aliyojiunga nayo mwaka 1986.
Tangu aanze kuifundisha Man United, Ferguson amesimamia michezo 1498 akiwa kocha; katika michezo hiyo ameshinda 894, suluhu 337 na kufungwa michezo 267. Maana yake ameshinda kwa silimia 60 kitu kinachomfanya kuwa kocha mwenye mafanikio makubwa kuliko wote Uingereza.
Aidha kwa kudhihirisha mafanikio yake Ferguson ametwaa mataji 49 tangu aanze kuwa kocha katika vilabu tofauti, ambapo mbali ya vikombe hivyo pia ameweza kujinyakulia tuzo zaidi ya 70 katika historia yake ya ufundishaji soka.
Akizungumza na vyombo vya habari wiki hii asubuhi Ferguson alisema kwa masikitiko kuwa, “maamuzi niliyofanya kustaafu ni miongoni mwa mambo niliyokuwa nikiyafikiria sana, nadhani ni wakati muafaka sasa kufanya hivyo.”
Kitu pekee ambacho kinamfanya Ferguson kustaafu kwa amani ni kuweza kuiwacha Man United katika daraja la juu la mafanikio hasa kwa kuvunja rekodi ya Liverpool kwa kuchukua kikombe cha ligi ya nchi hiyo kwa mara nyingi zaidi.
Kabla ya kujiunga na Manchester United, Ferguson alipata kuvifundisha vilabu vya East Stirling 1974, St Mirren 1975-78, Aberdeen 1978-86, baadaye akaifundisha timu ya taifa ya Scotland kwa mwaka mmoja halafu akahamia rasmi Manchester United tangu mwaka 1986 mpaka anastaafu kufundisha soka mwaka huu.
Ferguson ambaye amezaliwa Disemba 31, 1941 nchini Scotland alianza kucheza mpira wa miguu mwaka 1957 katika klabu ya Queens Park, baadaye akahamia St. Johnstone, Dunfermline Athletic, Rangers, falkrik na akamalizia na Ayr United mwaka 1974.
Akiwa anacheza safu ya ushambuliaji Ferguson katika vilabu vyote hivyo amefanikiwa kucheza michezo 317 na kushinda mabao 170.
Alijiunga Manchester Novemba sita baada ya kocha wa awali Atkinson kutimuliwa, katika mechi yake ya kwanza akiwa kocha Man United Ferguson alichapwa mabao 2-0 timu ya Oxford United Novemba 8, 1986 baadaye siku saba zilizofiuata alityoa suluhu tasa na timu ya Norwich City ikifuatiwa na ushindi wa kwanza wa bao 1-0 dhidi ya timu yake ya zamani QPR.
Kocha aliyekuwa akitajwatajwa kuchukua mikoba ya timu hiyo David Moyes wa Everton ndiye aliyetangazwa rasmi jana kuifundisha Man U baada ya Ferguson.

Aidha mechi ya mwisho ya Ferguson akiwa kocha man U itakuwa ni dhidi ya West Brom ambapo hiyo itakuwa ni mechi yake ya 1500 akiwa kocha katika timu hiyo, ingawa zipo taarifa kuwa mkongwe huyo amekubaliana na ombi la kubaki Man U akiwa mkurugenzi.

Wakati huohuo taarifa zinaeleza kuwa hisa za timu hiyo zimeshuka mara baada ya kocha huyo kutangaza kustaafu.

Taarifa za kustaafu kwa kocha wa Manchester United, Sir Alex Ferguson zimeifanya klabu hiyo kupoteza mapato yake.

Huku maelfu wa mashabiki wakionekana kushtushwa na habari za kustaafu kwa Fergie maarufu kama babu, lakini pia upande wa masoko kwa klabu ya Manchester United kumekuwa na pigo pia.
Hii ni baada ya kushuka kwa ununuzi wa hisa za klabu hiyo kwa zaidi ya asilimia tano kwenye soko la hisa la New York.
Wachambuzi wa masuala ya biashara wameeleza hofu yao juu ya kushuka kwa biashara za United kufuatia kuondoka kwa Ferguson kwa kusema itakuwa kazi kubwa kumpata mrithi wake ambaye ataweza kuchagiza mafanikio ya klabu hiyo yatakayovutia wadhamini mbalimbali kama alivyofanya kwa miaka 27 aliyokaa na United.
Familia ya Malcom Glazer yenye makao yake Miami nchini Marekani ambayo ndio inayomiliki klabu ya Manchester United bado haijatangaza mrithi wa Ferguson japo wadadisi na vyanzo vya karibu vya United vinasema huenda kocha wa Everton, David Moyes akakabidhiwa jukumu la kuifundisha United,taarifa ambazo hazijathibitishwa wala kukanushwa na uongozi wa Old Trafford.
Kushuka huko kwa hisa za United kumeifanya klabu hiyo kupoteza mapato yake kwa karibu asilimia 1.3 kwa hisa moja ambayo hununuliwa kwa dola za kimarekani 18.52 kwa hisa.
Licha ya kushuka kwa hisa hizo kufuatia taarifa za kustaafu kwa Ferguson lakini zaidi ya asilimia 30 ya hisa za United ziliuzwa kwenye soko la hisa hii leo.
BBC SWAHILI

No comments:

Post a Comment