Wednesday, May 1, 2013

Ligi kuu ya soka inaisha mashabiki wageuke wanachama ili kukuza uchumi wa vilabu vya soka nchini.

Kwangu kwa msimu huu kocha aliyeweza kuiletea mafanikio timu yake ni Mecky Mexime wa Mtibwa Sugar (wa kwanza kushoto).


Michuano ya ligi kuu Soka Tanzania bara maarufu Vodacom, inafikia tamati Mei 18 ikiwa tayari bingwa ameshajulikana na timu itakayoshika nafasi ya pili pia imeshajulikana.

Ugomvi mkubwa upo kwenye nafasi ya tatu, nne, tano na timu tatu zitakazoshuka daraja msimu huu, ili kuzipa nafasi timu za zilizopanda daraja kwa michuano ya msimu ujao.

Timu za Mgambo JKT, Toto Africa, African Lyon na Polisi Morogoro ndizo zilizo katika ‘Danger zone’ katika msimu huu kuaga michuano ya ligi kuu Tanzania bara.

Hata hivyo Mgambo JKT wana nafasi kubwa ya kubaki kwenye ligi kwani wamebakisha mechi tatu ambapo katika mechi hizo wanatakiwa kupata point moja tu ili waepukane na janga la kushuka daraja, ingawa wakipoteza michezo yote wataangukia katika orodha ya timu tatu zitakazoshuka daraja.

Lakini cha kusikitisha Mgambo JKT wamebakisha mechi ngumu tupu kati ya Yanga, Azam na African Lyon ambao ni mahasimu wao katika kushuka daraja.

Kumalizika kwa ligi ni kitu kimoja lakini maandalizi ya msimu ujao wa 2013/14 ni kitu cha msingi sana kwa timu zinazoshiriki hasa zile ambazo matarajio yao hayakutimia katika msimu unaoisha.

Ipo haja mashabiki kuanza kugeuka wanachama ili kuzipa nguvu timu zao, mashabiki wasiishie tu kupiga kelele bali wawe wanachama hai watakaonunua kadi na kuzichangia timu kiuchumi ili kutimiza malengo ya vilabu vya soka nchini.

Nikiambiwa nitaje timu tatu zilizofanya vizuri msimu huu nitazitaja timu za Azam FC, Mtibwa Sugar na Kagera Sugar; timu hizi zimeongeza upinzani mkubwa katika soka la Tanzania hata katika kuitwa timu ya Taifa, utaona ule ‘usimba’ na ‘uyanga’ umepungua lakini Mtibwa Sugar na Azam FC ndizo timu zinazoongoza kuwa na wachezaji wengi walioitwa katika vikosi vyote viwili vya kocha Kim Poulsen anayenoa Taifa Stars na Young Tafa Stars.

Kitu kingine nilichojifunza kwenye msimu huu ni matumizi bora ya timu za vijana kwenye vilabu, wazo hili lilipoletwa na Rais wa TFF Leodger Tenga, watu walilichukulia kurahisi, lakini kampuni ya Azam kupitia maji ya Uhai ilipoanzisha michuano ya timu za vijana chini ya miaka 20 vilabu havikuchukulia uzito michuano hiyo.

Hata hivyo michuano iliyopita mwanzoni mwa mwaka huu imeibua vipaji lukuki ambavyo vimeleta faida kubwa kwa timu za Simba na Coastal Union. Mpaka sasa Simba inatembea kifua mbele kutokana na vijana wa timu B, na Coastal Union kadhalika.

Hivyo vilabu vitilie mkazo sana kuibua vipaji vya vijana ili ligi irudi ilipotoka kwa kujivunia wachezaji wa ndani, vilabu vingi viliwika miaka ya nyuma kwa kutumia wachezaji wazalendo na wacheaji watapatikana kwa kukuza vipaji vya watoto.

Lakini timu kubwa nazo ziache kupora wachezaji kutoka timu zilizo na uchumi mdogo kwa hadaa, hii itapunguza ushindani. Kwani historia inaonyesha mara nyingi wachezaji wanapokwenda kucheza timu kubwa hawadumu katika vipaji vyao na hii inatokana na hujuma wanazofanyiana na mara zote mhanga wa hujuma hizi anakuwa ni mchezaji asiye na hatia.

Maana tayari timu kubwa zimeshaanza kutajataja wachezaji watakaowasajili msimu ujao, si jambo baya lakini watumie taratibu zilizowekwa kuzungumza na timu badala ya kuwaghilibu wachezaji kwa kuwaonyesha fedha nyingi ili wavunje mikataba na timu zao.
 HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
1st May, 2013

No comments:

Post a Comment