Friday, May 10, 2013

Yanga kutosherehekea ubingwa ikiwa hawatoifunga Simba Mei 18.

 Katibu wa Wazee wa Yanga Mzee Ibrahim Akilimali, akiandaa nyaraka ili kutoa tamko la wazee kuhusu mechi yao dhidi ya Simba Mei 18 mwaka huu.

 Hapa mzuka wa Mzee Akilimali ukiwa umepanda anaanza kuzungumza kwa ishara na sauti ya juu.

Hapa akiweka msisitizo.


Na Hafidh Kido

Mabingwa wa soka Tanzania bara Dar es Salaam Young Africans, wametangaza kutofanya sherehe ikiwa watafungwa na watani wao wa jadi wekundu wa msimbazi Simba katika mechi itakayowakutanisha uwanja wa taifa Mei 18.

Katika mechi hiyo yenye ushindani mkubwa ambayo ndiyo itafunga pazia la ligi kuu ya soka vodacom Tanzania bara, Yanga wamejitapa kuwafunga Simba kwa idadi ya mabao ambayo hawakuyataja lakini wakiweka wazi kuwataka waamuzi wa mechi hiyo kufuata sheria 17 za mchezo huo.

Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya klabu hiyo leo mchana katibu wa wazee wa Yanga, Mzee Ibrahim Akilimali alisema katika mchezo huo lazima wawachinje wapinzani wao ili kuongeza furaha ya ubingwa.

Kwanza tunawashukuru viongozi wetu kwa kutuongoza vema mpaka tumenyakua ubingwa msimu huu, wanachama na wachezaji wana imani kubwa na uongozi wao. Lakini ili kuongeza furaha ya ubingwa huu lazima katika mchezo wa Mei 18 tuwachinje Simba ili tusherehekee kwa shangwe na vigelegele.

“Mwenye macho haambiwi tazama timu yetu ni timu bora kuliko timu zote msimu huu, lakini tunaomba kitu kimoja waamuzi watakaochezesha mchezo huo wanatakiwa kutumia sheria 17 za soka na tunaahidi tutawafunga kwa kiasi tunachokitaka,” alisema mzee Akilimali kwa sauti ya kujitapa.

Aidha wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari Mzee Akilimali aliyezungumza kwa niaba ya mwenyekiti wa wazee wa Yanga, Alhaj Jabir Makatundu alisema mchezo wa msimu uliopita dhidi ya watani wao ulijawa na mizengwe mingi pamoja na kukosa umakini kwa waamuzi kiasi wakafungwa mabao matano, lakini msimu huu Simba wasitegemee makosa yale yatajirudia.

“Ule mchezo wa msimu uliopita haukuchezeshwa ‘fair’ haiwezekani mchezo mmoja uwe na offside 18, Yanga tulionekana tumeotea mara nyingi zaidi mpaka wale watangazaji wa Supersport walishangaa, ndipo wakaambiwa hao ni Simba na Yanga mambo kama hayo ni ya kawaida.

Mjumbe mwingine mzee Hashim Mwika aliongeza kuwa msimu uliopita Yanga walifungwa na Simba kwasababu wazee hawakuwa radhi na uongozi ndiyo maana laana yao ikawafanya wachezaji wasiwe na umakini uwanjani.

“Wazee tulivua kofia ndiyo maana Yanga ilikubali kipigo cha mabao mengi kiasi kile, wazee tuliiwachia radhi klabu lakini msimu huu tupo vizuri na kila idara inashirikiana vilivyo kuhakikisha tunafanya vizuri,” alisema.

Katika hatua nyingine mzee Akilimali anayefahamika kwa vituko alipoulizwa swali na KIDOJEMBE juu ya wapinzani wao kuweka kambi Zanzibar alijibu; “Huo ni uoga, uoga ndiwo unaowafanya kuweka kambi Zanzibar, sisi tutabaki hapahapa Dar es Salaam tena tutaweka kambi yetu hapahapa klabuni hatuogopi kitu, na tukifungwa na Simba hata hiyo sherehe yenyewe hatufanyi itakuwa haina maana.”

Msimu uliopita yanga ilimaliza ligi ikiwa nafasi ya tatu nyuma ya mabingwa Simba na Azam FC walioshika nafasi ya pili. Kitu kilichoibua simanzi kubwa ni pale Simba walipochukua ubingwa kwa mbwebwe na kuwafunga watani wao mabao 5-0.

Mabao hayo yameonekana kuwapa kiwewe Yanga hasa ikizingatiwa walikuwa na migogoro ya kiuongozi, lakini msimu huu Yanga wamejipanga vizuri wakatangaza ubingwa mapema na kuwaacha watani wao wakigombania nafasi ya tatu huku nafasi ya pili ikikaliwa na Azam FC walewale.

HAFIDH KIDO
Kidojembe @gmail.com
+255 713 593894
+255 752 593894
DAR ES SALAAM, TANZANIA
10 MEI, 2013

No comments:

Post a Comment