Sunday, May 12, 2013

Kifaa cha kurahisisha upatikanaji wa chanjo ya UKIMWI chagundulika.



Dar es Salaam. Wanasayansi nchini Marekani wamebaini kifaa kipya kitakachoharakisha upatikanaji wa chanjo ya virusi vya Ukimwi (VVU).
Taarifa kwa Mwananchi Jumapili iliyotolewa Alhamisi wiki hii na Taasisi ya Tafiti Kukabiliana na Magonjwa ya Mzio na Kuambukiza (NIAID) ya nchini Marekani ilieleza kuwa mfumo wa kifaa hicho siyo tu utasaidia kurahisisha chanjo kukabiliana na VVU, bali hata kwa magonjwa mengine yanayosababishwa na virusi kama mafua na yale yanayosababisha uvimbe wa ini.
“Ni mfumo wa hali ya juu wenye uwezo wa haraka wa kuchambua chembechembe kinga zenye uwezo wa kuangamiza aina mbalimbali za VVU zinazopatikana duniani,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Taarifa hiyo iliyoambatanisha majina ya wanasayansi nguli wa NIAID ambao wamethibitisha kifaa hicho chenye mfumo mpya katika teknolojia ya kuchambua VVU, umeweka wazi kuwa matatizo waliyokuwa wakipata wanasayansi katika kudhibiti virusi sasa imepata ufumbuzi.
Uzuri wa kifaa hicho unaelezwa kwamba ni kuweza kuchambua na kutofautisha chembe kinga za aina mbalimbali, hata kujua idadi na uwezo wake katika kushambulia adui katika mwili wa binadamu.
“Uchambuzi wa kifaa hiki unaweza kutumika kuchunguza namna mwili wa binadamu unavyoweza kukabili maradhi mengine yanayosababishwa na virusi kama vile mafua na uvimbe wa ini,” anaeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Wanasayansi nguli wa NIAID waliothibitisha uwezo wa kifaa hicho ni Mtaalamu wa Dawa na Mifumo ya Kibiolojia, ambaye pia ni Mkuu wa Idara ya Chanjo, Profesa Peter Kwong na Mkuu wa Idara ya Kinga, Profesa John Mascola.
Wataalamu hao wanaeleza kuwa kifaa hicho kina uwezo wa kutofautisha ni chembechembe gani za kinga zenye uwezo wa juu katika kukabili virusi vya maradhi.
Kupitia njia hiyo, inaelezwa kuwa ni rahisi kubaini chanjo yenye nguvu, hivyo kuharakisha upatikanaji wa chanjo itakayothibitishwa kukabiliana na VVU.
Kulingana na teknolojia na tafiti mbalimbali, VVU bado hajaipata tiba au chanjo madhubuti, ingawa wameweza kupata dawa zenye uwezo mkubwa wa kupunguza makali ya virusi hivyo (ARVs).
Hadi sasa tafiti mbalimbali zimeonyesha uwezekano wa kupatikana tiba na chanjo katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Kwa sasa tafiti nyingi zipo kwenye majaribio, NIAID inaeleza kuwa kupatikana kwa kifaa hicho kutaharakisha kazi ya kuchanganua uwezo wa chanjo hizo katika kukabiliana na VVU.
Taasisi hiyo ya utafiti inaeleza kuwa mfumo wa kifaa kilichokuwepo awali, haukuwa na uwezo wa kuchambua kiufasaha chembe kinga mbalimbali wala umahiri katika kukabiliana na virusi.
“Hata hivyo, kwa sasa itakuwa rahisi kuchambua sampuli za damu, hata kutofautisha makabiliano dhidi ya virusi kulingana na makusudio yetu.
Awali hatukuwa na teknolojia ya kufanya hivyo,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo ya NIAID.
Kwa jinsi kifaa hicho kinavyofanya kazi, walikifananisha na mashine ya kutambua alama za vidole kinachoweza kutofautisha watu bila kukosea.
Kulingana na taarifa ya watafiti hao, kifaa hicho kina uwezo wa haraka wa kufanya kazi hata kwa kutumia kiwango kidogo cha damu, kuliko njia nyingine zozote.
Ugonjwa wa Ukimwi iligundulika miaka 30 iliyopita, hadi sasa umeua watu wengi na kusababisha kupungua kwa nguvukazi pamoja na wataalamu wa sekta mbalimbali hasa katika nchi maskini.
Kauli ya Serikali
Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid ameelezea kuwa ugunduzi huo ni ukombozi kwa dunia katika kuharakisha upatikanaji wa chanjo ya VVU.
“Ni jambo zuri hasa katika kuharakisha upatikanaji huo wa chanjo… Maana virusi (VVU) hawa wamekuwa na tabia ya kubadilikabadilika, hata kufanya iwe kazi ngumu kupata antibodies (chembe kinga) watakaosaidia mwili kupambana na virusi wa Ukimwi,” alisema Dk Rashid.
Alikiri kuwa zipo tafiti mbalimbali za chanjo ya Ukimwi duniani, lakini zimekuwa zikisuasua kutokana na ugumu wa vifaa madhubuti vya kuchunguza mwenendo wa chembe kinga, hata uwezo wake, hivyo kazi hiyo kuchukua muda mrefu.
Dk Rashid akasema, ugunduzi kama huo ni muhimu kwa wakati huu ambapo kuna juhudi za kutafuta tiba na chanjo ya Ukimwi.
Kuhusu juhudi za Serikali kupata kifaa hicho ili kuharakisha shughuli za utafiti nchini, Dk Rashid alisema kuwa taratibu zake ni hadi pale kitakapothibitishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO).
Alisema vifaa vyovyote vinavyohusiana na tiba vinaweza kuingizwa nchini baada ya kupata maelezo na umuhimu wake katika kulisaidia taifa kwa uthibitisho wa WHO.
Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi (Tacaids) Dk Raphael Kalinga alisema iwapo wanasayasni hao watakuwa wamefanikiwa katika hilo ni mafanikio katika teknolojia ya kukabiliana na VVU.
“Ni hatua nzuri,” alisema Dk Kalinga akisisitiza kuwa ni jambo linaloinufaisha dunia na hakuna anayeweza kukataa maendeleo.
Pamoja na pongezi hizo, Dk Kalinga alisema ugunduzi wa aina hiyo utasaidia zaidi, hasa uchunguzi kwa watoto wachanga, ambao kazi yake imekuwa ngumu ukilinganisha na watu wazima.
MWANANCHI

No comments:

Post a Comment