Tuesday, May 7, 2013

Pinda atoa ripoti ya alichokiona Arusha...


Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda, amewataka viongozi wa kisiasa kuacha kuweka ushabiki kwenye tukio la bomu lililotokea Arusha mwishoni mwa wiki iliyopita katika kanisa katoliki.

Akitoa ripoti ya tukio hilo bungeni mjini Dodoma leo mchana baada ya kutembelea eneo la tukio Pinda alisema tukio hilo ni baya na la kushitusha hivyo kuwataka watanzania kuwa watulivu na kuwaombea majeruhi wapone haraka badala ya kuanza kutupiana lawama.

“Ni tukio kubwa, kitendo kibaya kisichofurahisha hata kidogo na mambo makubwa kama haya tusiingize siasa wala rusiingize ushabiki tuwape moyo ndugu zetu wa Arusha. Kwa bahati mbaya wamepitapita viongozi wa kisiasa kule badala ya kuwafariji wahanga wameingiza visiasa,”alisema Pinda.

Awali akitoa taarifa hiyo wakati wa mjadala wa bajeti ya wizara ya mambo ya ndani Waziri Mkuu alisema katika wagonjwa 66 waliopelekwa hospitali ya Mount Meru tayari wagonjwa watatu wamefariki dunia na wagonjwa 24 wamesharuhusiwa.

Akizungumzia watuhumiwa wanane waliotiwa mbaroni kuhusiana na tukio hilo Pinda alisema, “uchunguzi bado unaendelea, mpaka sasa jeshi la polisi linawashikilia watuhumiwa wanane wane kutoka uarabuni, watatu ni raia wa Tanzania akiwemo Joseph na Victor Ambroz. Hawa raia wa kigeni walikamatwa wakiwa njiani kuelekea Nairobi tunaendelea kuwafanyia mahojiano ili kubaini chanzo ni nini, na tunawaomba watu wa Arusha watupe ushirkiano katika hili ikiwa kuna mtu mwenye taarifa zozote.”

Mbali ya Waziri Mkuu kiongozi mwingine aliyetembelea eneo la tukio ni makamu wa Rais Dk Mohammed Gharib Bilal ambaye alikwenda siku hiyohiyo ya tukio, kiongozi mwingine anayetarajiwa kufika jijini Arusha ni Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete aliyekatisha ziara yake nchini Kuwait, kiongozi mwingine ni makamu wa kwanza wa Rais Zanzibar Seif Sharif Hamad.

Katika tukio hilo bomu la kurusha kwa mkono lilitupwa katika kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti wakati ibada ya uzinduzi wa Parokia hiyo ambapo mgeni rasmi alikuwa ni balozi wa Vatican nchini Askofu Francisco Mantecillo Padilla aliyekuwa mwenyeji wa Askofu Josephat Lebulu wa kanisa hilo jimbo la Arusha.

HAFIDH KIDO
7th May, 2013
Dar es Salaam, Tanzania

No comments:

Post a Comment