Friday, July 13, 2012

Haya someni nilichowaahidi jana.

                                    Picha hii jembe nikiwa chumbani kwangu Chuoni. Kansanga, Kampala, uganda


Ndugu zangu

Jana niliwaahidi kuwa nitawapa kisa kimoja nilichotoa ahadi kwa rafiki yangu Evans namna nitakavyopambana na umaskini. Naam raha ya ahadi ni kuitimiza na si vinginevyo.

Tukiwa chuoni tulikuwa na mawazo mengi sana namna tutakavyokabiliana na maisha ya mtaani, chuoni kweu tulikuwa na wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali Afrika, lakini watanzania tulikuwa na urafiki mkubwa na wakenya. Nadhani Kiswahili kimetuunganisha si unajua watanzania kingereza tatizo?

Sasa nilijenga urafiki mkubwa na ndugu Evans Musoka Luseno, Mkenya huyu mwenyeji wa Nairobi, urafiki wetu ulitokana na kufanana malengo. Katika maisha hakuna kitu kizuri kama kuwa na rafiki mnaefanana malengo.

Hivyo mwenzangu aliamua akimaliza chuo siku akirudi Nairobi kutoka Kampala moja kwa moja atafikia kwake na si kwao. Kwakuwa mimi ninakaa na mzazi wangu wa kike katika nyumba ya kaka yangu hivyo sikupanga kuhama nyumbani maana nyumba ni kubwa na kuhama kwangu itakuwa ni kukimbia majukumu wala si kuanza maisha mapya.

Mimi nilimuahidi rafiki yangu yule kuitendea haki shahada yangu ya mawasiliano ya umma, na hasa niliamua kujikita katika uandishi wa makala katika magazeti ili nipate malipo yatakayoniwezesha kumlea mama yangu. Nilifanya hivyo baada ya kurudi na nikawa ninaandika makala nyingi iwezekanavyo katika magazeti, tatizo likaja kwenye malipo. Sikuwa nikipata chochote kwa makala zile ‘nilikopwa.’

Mwezi uliopita nilikwenda mjini Kampala kufuatilia matokeo yangu na namna ya kuendelea na shahada ya pili (master degree), nikiwa njiani kurudi nyumbani nilimtembelea rafiki yangu Musoka na pia nilipanga kupata nafasi ya kukutana na wangu wa ubani, naam shemeji yenu ni mkenya.

Nilishitushwa sana na mafanikio aliyoyapata ndugu yangu yule, ana nyumba ya vyumba viwili, choo na jiko ndani, analipa takriban elf kumi ya Kenya kwa mwezi. Si pesa ndogo kwa Tanzania.

Tulizungumza mambo mengi na nilishituka zaidi niliposikia hana kazi ya kuajiriwa ila ni mjasiriamali, ana bodaboda na baadhi ya miradi. Mwisho wa wiki anakwenda kuchekesha (Standup comedy) na anapata senti za kujikimu. Kadhalika anakwenda katika stesheni ya televisheni na kujitolea kufanya kazi (volunteering).

Tulizungumza mambo mengi sana na niliona haya kwa kutotekeleza hata kimoja katika tulivyoahidiana nilijisikia uchungu sana pale aliponambia hana msaada wowote kutoka kwa ndugu yake na kama haitoshi yeye ndie anaemsaidia mama yake. Kwa pamoja tuliamua tupange upya mikakati yetu,na tulipanga tuwasiliane na dada Monica Akech mwanafunzi kutoka Uganda tuliwahi kusoma nae ili tuanzishe jarida ‘magazine’ ya east Africa, itakayobeba mambo kutoka kila kona ya nchi tatu hizi.

Baada ya kurudi nyumbani na kuona mambo bado nimagumu katika kuanzisha jarida hilo nikaamua kwanini nisianzishe jarida la kwenye mtandao? Ndipo nikapata wazo hili la kuanzisha blogu ya kijamii.

Hivyo naamini huko aliko Nairobi, rafiki yangu ameanza kuona juhudi zangu nami najisikia faraja sana kwa kukamilisha ndoto yangu hii. Nafarijika kwa mafanikio ninayoendelea kuyapata na nafurahi kuona blogu yangu imekuwa chanzo cha habari za watu wengu kutoka nchi zifuatazo idadi ya watu wanaotembelea kwenye mabano, USA (970), Tanzania (193), Russia (49), UK (29), Kenya (19), Bahrain (4), Oman (4) na Germany (1).

Na leo asubuhi saa nne nilishatembelewa na watu 51, ambao kwa siku za awali hao walikuwa wakitembelea kwa siku tatu. Jana nilitembelewa na watu 310 na jumla ya watu wote wanaotembelea tangu blogu ianzishwe ni watu 2584.

Hii ni hatua kubwa sana na ninamshukuru Mungu kwa kila jambo. Nimeandika haya si kwa kutaka sifa bali ni kukupa moyo wewe unaesoma kuwa kila kitu kinawezekana usivunjike moyo, anza sasa kutimiza ndoto yako, kesho haijawahi kuonekana, hivyo huijui.

HAFIDH KIDO
0713 593894/ 0752 593894
DAR ES SALAAM, TANZANIA
hafidhkido@yahoo.com

No comments:

Post a Comment