Thursday, August 16, 2012

Mizengo Pinda aahirisha bunge leo mpaka mwezi Octoba..


Na Hafidh Kido

Leo bunge limeahirishwa mpaka mwezi octoba mwaka huu, utakumbuka kikao cha bajeti ambacho ndicho kikao kirefu kuliko vikao vyote kilianza tarehe 12 June mwaka huu mpaka leo tarehe 16 August leo.

Shilingi trilioni 15.19 zimepitishwa kuwa bajeti ya mwaka mzima kwa mwaka wa fedha 2012-2013 ambapo kwa mujibu wa waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda, alisema shilingi trilioni 10.60 zitatumika kwa matumizi ya kawaida kama mishahara na kulipa madeni, halafu shilingi trilioni 4.59 zitatumika kwa shughuli za maendeleo.

Aidha Waziri mkuu Pinda alitaja vipaumbele vya Serikali katika matumizi ya fedha hizo kwa mwaka huu wa fedha kuwa ni  miundombinu, kilimo, viwanda, maendeleo ya rasilimali watu na huduma za utalii biashara na uchumi.

“Katika mwaka huu wa fedha serikali imeainisha vipaumbele vitano ambavyo ni sekta ya miundombinu kama barabara, madaraja na mawasiliano, kipaumbele cha pili ni kilimo ambapo itahusisha mifugo na uvuvi, kipaumbele cha tatu ni maendeleo ya viwanda hasa tukiangalia vile viwanda vinavyozalisha bidhaa zake kwa kutumia bidhaa za ndani.

“Aidha Kipaumbele cha nne ni  maendeleo ya rasilimali watu tukiangalia sana ajira na maendeleo ya mtu mmoja mmoja, na kipaumbele cha tano ni huduma za utalii, biashara na uchumi. Tumehakikisha ndani ya mwaka huu wa fedha vipaumbele vyote hivyo vimepata mafungu ya kutosha kuweza kutimiza malengo ya Serikali,” alisema Pinda.

Hata hivyo katika hotuba yake hiyo ya majumuisho ya kikao cha bajeti Pinda alisema Serikali itahakikisha hakutakuwepo matumizi mabaya ya fedha ili kuweka nidhamu ya matumizi.

Waziri mkuu aliongeza kuwa ili kulinda matumizi mabaya ya fedha Serikali itapima uwajibikaji kwa watendaji wake na kuhakikisha inapunguza matumizi ya anasa kama kununua magari ya gharama, posho za vikao, warsha na safari za nje zisizo na tija.

Aidha katika kuhakikisha Serikali inapunguza baa la njaa Waziri Mkuu pinda alisema watatoa tani laki moja katika ghala ya chakula ya taifa ili kupeleka katika mikoa ambayo imekumbwa na baa la njaa kwa kipindi cha hivi karibu.

Katika suala la miundombinu Pinda alisema kuwa wakala wa barabara nchini (Tanroads) wamepewa bil 580 ili kuhakikisha wanakamilisha miradi 14 ya barabara katika mikoa yenye matatizo ya msongamano wa magari na miundombinu inayoleta usumbufu kwa maendeleo. Pesa hizo zitatumika kujenga madaraja kama la kigamboni, barabara za kuzunguka na barabara za juu (fly overs).

Aidha katika mambo ya msingi ambayo Serikali imeyafanya kwa bajeti hii ni kukaribia lengo la kufikisha asilimia 15 ya bajeti katika wizara ya afya. Kwani kwa mujibu wa Waziri Mkuu Pinda, jumuiya ya Afrika ilikutana kujadili suala la kutoa kipaumbele kwa wizara za afya kwa kuhakikisha bajeti za wizara hizo katika nchi za Afrika zinafika asilimia 15 ya bajeti ya jumla ili kujenga taifa lenye afya.

“Katika vitu ambavyo tunajivunia kwa najeti ya mwaka huu wa fedha ni kukaribia lengo la kuwa na asilimia 15 ya bajeti katika wizara ya afya, ambapo kwa mwaka huu asilimia 10 ya bajeti tumeipeleka katika wizara ya afya, hivyo tumebakisha asilimia tano tu tufikie lengo,” alisema.

Nae spika wa bunge la Tanzania Anne Makinda alihitimisha kikao cha leo kwa kuwataka wabunge kuwa watulivu na kuacha kuingilia kazi ya kamati ya bunge iliyoundwa ili kuchunguza kashfa ya rushwa inayowakabili wabunge ambao inadaiwa walichukua rushwa katika shirika la umeme nchini Tanesco ili kupitisha tenda ya uuzaji mafuta kutoka kampuni ya mafuta ya puma energy.

“Kamati hii inafanya kazi zake kama mahakama, hivyo kuanza kuzungumza mambo yanayohusu sakata hilo mkiwa majimboni ni sawa na kuingilia mwenendo wa shauri hili nayo ni makosa. Hivyo nawaomba wabunge muwe watulivu na kuacha ushabiki,” alisema Spika Makinda na kuahirisha bunge mpaka mwezi Oktoba mwaka huu.

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
16/08/2012
kidojembe@gmail.com 

No comments:

Post a Comment