Saturday, December 15, 2012

Azam waharibiwa kisaikolojia wawasili Congo bila ya kocha na msaidizi wake...

 Kocha wa Azam FC mwingereza Stewart Hall.... ambae ameachwa Nairobi pamoja na msaidizi wa Kali Ongala ambao pasi zao za kusafiria zilionekana ni za Uingereza.

Wachezaji wa Azam FC wakikaguliwa pasi zao za kusafiria mara baada ya kuwasili uwanja wa ndege wa Kinshansa...


Na Mahmoud Zubeiry, Kinshasa
WAWAKILISHI wa Tanzania katika Kombe la Shirikisho la Soka Afrika, (CAF), Azam FC wamewasili salama mjini Kinshasa, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) majira ya saa 5:58 usiku wa jana kwa saa za huku na saa 7:58 kwa saa nyumbani Tanzania, tayari kucheza mashindano ya Kombe la Hisani mjini hapa.
Hata hivyo, Azam wamewasili pungufu ya watu watano katika msafara wao wa watu 27, kufuatia maofisa na wachezaji wa kigeni kuzuiliwa mjini Nairobi, Kenya kwa kutokuwa na viza za kuingia DRC.
Wenyeji wa Azam, waandaaji wa mashindano waliwahakikishia wageni wao hakutakuwa na tatizo la kuingia DRC bila viza, kwa kuwa wamekwishaandaa utaratibu mzima na msafara mzima utapatiwa viza mara utakapowasili Kinshasa.
Hata hivyo, kwa ujumla hali ilikuwa tofauti, Kocha Mkuu Stewart Hall, Msaidizi wake, Kali Ongala, wote raia wa Uingereza, Daktari Paulo Gomez, raia wa Ujerumani na wachezaji Kipre Tcheche na Kipre Balou raia wa Ivory Coast walizuiwa mjini Nairobi.
Mkuu wa msafara, Katibu wa Azam, Nassor Idrisa alitumia busara kwa kuwapatia fedha za malazi na kujikimu watu hao watano ili wabaki Nairobi kushughulikia viza na wataungana na timu leo baadaye.
Aidha, baada ya kufika Uwanja wa Ndege wa Njili mjini hapa, msafara wa Azam pia ulipata misukosuko mingine, kuanzia uwanjani hapo, wakati Maofisa wa Idara ya Uhamiaji walipokataa kuupokea kwa sababu ya viza.
Ilifikia hatua Maofisa hao wakaagiza msafara urejeshwe kwenye ndege ili kurejea Tanzania, kwa kuwa haukuwa na viza, hata hivyo wenyeji wa mabingwa hao wa Kombe la Mapinduzi, wakafanya jitihada na kufanikiwa kumalizana na Maofisa hao wa Idara ya Uhamiaji.
Kufika katika hoteli ya Florida walipopangiwa kufikia, lilikuwa ni tatizo lingine, kwanza chakula kilikuwa kichache na baadhi ya wachezaji walilala bila kula kabisa. Lakini kwa ujumla mazingira ya hoteli hayakuwa yenye kuridhisha.
Hata hivyo, kwa mara nyingine Katibu, Nassor akatumia busara kwa kukubali timu ilale hadi asubuhi na kupatiwa na hoteli nyingine yenye hadhi, jambo ambalo wenyeji wao waliafiki na kuomba radhi kwa usumbufu wote uliojitokeza.
Katika michuano hiyo, Azam inatarajiwa kufungua dimba leo kwa kumenyana na Dragons kwenye Uwanja wa Martyrs, saa 9:30 za huku, yaani saa 11:30 za nyumbani Tanzania.
Azam ambao ni washindi wa pili wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame na Ligi Kuu, wamepangwa katika Kundi B pamoja na Dragons na Shark FC, ambayo watacheza nayo Desemba 17.
Ikifuzu kwenye kundi lake, Azam itaingia Nusu Fainali moja kwa moja, ambazo zitachezwa Desemba 25 na Desemba 26 itakuwa Fainali na mechi ya kusaka  mshindi wa tatu.  Kundi B, lina timu za DC Motema Pembe, Diables Noirs, FC MK na Real De Kinshasa.  Katibu wa Azam FC, Nassor Idrisa amesema wamekuja kushiriki mashindano haya kwa lengo la kuwapa mazoezi na uzoefu wachezaji wake kabla ya kuingia kwenye Kombe la Shirikisho mwakani.
Alisema Azam pia, itatumia mashindano hayo kama fursa ya kuwapima wachezaji wake kabla ya kuanza kwa Kombe la Shirikisho mwakani, ambako wamepangwa kuanza na Al Nasr Juba ya Sudan Kusini.
Kikosi cha Azam kilichowasili jana hapa, ukiondoa waliozuiwa Nairobi ni; Mwadini Ally, Jackson Wandwi, Gaudence Mwaikimba, Himidi Mao, Ibrahim Mwaipopo, Jabir Aziz, Luckson Kakolaki, Samir Hajji Nuhu, Zahoro Pazi, Seif Abdallah, Malika Ndeule, Omar Mtaki, Abdi Kassim, Uhuru Suleiman, Brian Umony na David Mwantika.
Wachezaji wengine ambao hawahusiki katika safari hiyo, ni wale waliopo kwenye kikosi cha timu ya taifa, Khamis Mcha ‘Vialli’, John Bocco ‘Adebayor’ na Salum Abubakar. Wachezaji wapya, Joseph Mieno na Joackins Atudo kutoka wanaweza kujiunga na timu baadaye mjini hapa.
Katika mchezo wa leo, timu itaongozwa na kocha wa makipa, Iddi Abubakar Mwinchumu ambaye ni ‘Azam Damu’, aliyeipandisha timu kutoka Daraja la Tatu hadi Ligi Kuu kwa kulinda lango vema, huku John Bocco ‘Adebayor’ akitupia nyavuni.

 Chanzo: Bin Zubeiry blogspot....

No comments:

Post a Comment