Wednesday, December 26, 2012

Kikosi cha Coastal Union B ni kikosi bora vijana chini ya miaka 20 Tanzania.




Na Hafidh Kido

Michuano ya Uhai Cup iliyokuwa ikishirikisha vijana chini ya miaka 20 kwa timu zinazoshiriki ligi kuu ya soka Tanzania bara imekamilika rasmi jumapili tarehe 23, Desemba wiki iliyopita kwa Azam FC kutawazwa mabingwa baada ya kuifunga Coastal Union kwa penalt 3-1 baada ya dakika 120 kuisha kwa sare ya 2-2.

Hakika Rais wa shirikisho la mpira wa miguu nchini TFF Leodger Tenga anastahili pongezi kwa kuanzisha utaratibu wa kuweka sheria inazozibana timu zinazoshiriki ligi kuu kuwa na timu ndogo za vijana wa chini ya miaka 20. Utaratibu huu lengo lake ni kuibua vipaji vya vijana ambao awali walikuwa wakiishia kucheza timu za shule na kubaki mitaani bila kuonekana katika dunia ya michezo.

Kanali Iddi Kipingu aliekuwa mwalimu mkuu wa shule ya sekondari Makongo ndie aliekuwa wa kwanza kusaidia vijana kwa kuwachukua kutoka katika michuano ya shule za sekondari na msingi maarufu UMISETA na UMITASHUMTA aliwaingiza katika shule yake halafu anawasomesha bure huku akiwakuza vipaji vyao.

Utaratibu wake huu ulisaidia kuibua vipaji vya wachezaji waliokuja kusumbua sana katika soka la Tanzania, miongoni mwao ni kipa namba moja wa Taifa Stars Juma Kaseja, wachezaji wengine hatari kama Bonifas Pawasa, Nico Nyagawa, Renatus Njohole na Haruna Moshi ‘Boban’. 

Lakini kwa sasa ni lazima kwa timu yoyote ya ligi kuu kuwa na timu ya vijana, kama timu itakwenda kinyume na utaratibu huu inaweza hata kuondolewa kwenye michuano; zamani timu kubwa tu kama Simba na Yanga ndizo zilizokuwa na timu B ambapo walizitumia kuvuna wachezaji wapya kwa matumizi ya baadae ingawa haikuwa lazima kufanya hivyo.

Coastal Union B ina miaka mitatu tangu ianzishwe, nimekuwa nikifuatilia maendeleo yao nimegundua ni timu yenye vijana wenye vipaji vya hali ya juu ingawa hawana kambi rasmi ‘Academy’ kama wanavyofanya Azam FC, Simba SC na Yanga ambazo ndizo timu zinazofanya vizuri katika ligi kuu ya bara.

Kudhihirisha hayo siku ya fainali iliyowakutanisha Coastal Union kutoka Tanga na Azam FC ya jijini Dar es Salaam, meneja wa Azam FC Said Salim Bakhresa ambae pia yupo katika kamati ya maandalizi ya michuano hiyo, alipopata nafasi ya kusema chochote hakusita kukimwagia sifa kikosi cha Coastl Union chini ya miaka 20 kuwa ni kikosi bora katika michuano hiyo.

“Niwashukuru sana sana tena sana viongozi wa Coastal Union kwa kuweza kuwalea vijana hawa mpaka kuweza kucheza soka katika kiwango cha juu kama hiki, hakika sikutegemea kama wangeweza kucheza namna hii. Walistahili kushinda mchezo huu lakini bahati haikuwa yao ila nikiri tu Coastal Union chini ya miaka 20 ni timu nzuri ya vijana niliyowahi kushuhudia hapa nchini,” Bakhresa.

Si hao tu hata Kanal mstaaf Iddi Kipingu na Leodger Tenga kwa vipindi tofauti waliimwagia sifa Coastal Union kwa kuweza kuwaandaa vijana wao na kuweza kutoa burudani ya hali ya juu.

Katika michuano hiyo Coastal Union hawakupoteza mchezo hata mmoja katika michezo sita waliyocheza ambapo minne katika makundi miwili ni ya robo na nusu fainali. Katika michezo yote hiyo walionyesha soka la hali ya juu hasa katika robo fainali walipokutana na Ruvu Shooting uwanja wa Chamanzi, mpaka wanakwenda mapumziko Coastal walikuwa nyuma kwa magoli mawili.

Lakini waliporejea kwa kipindi cha lala salama vijana wa Coastal Union walifanikiwa kurudisha magoli yote mawili na kuingia hatua ya penalt ambapo walifanikiwa kusonga mbele baada ya kushinda penalt 4-3. katika hatua ya nusu fainali walikutana na Simba SC hiyo ndiyo mechi iliyokuwa ikiwasumbua kichwa, maana Simba walikuwa mabingwa watetezi wa michuano hiyo na waliaminika kucheza soka la kuvutia.

Lakini hali ilikuwa tofauti na vijana wa Simba walikubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa vijana wa Coastal Union hivyo kuvuliwa ubingwa rasmi na kuiwezesha Coastal Union kutinga fainali ya michuano hiyo kwa mara ya kwanza.

Azam ndiyo iliyokuwa ya kwanza kuingia fainali baada ya kuitoa Mtibwa Sugar kwa mikwaju ya penalt 3-2. Ambapo matokeo ya dakika 90 za kawaida yalikuwa ni 1-1.

Katika fainali iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu hasa ikizingatiwa Azam FC wanasifika kwa soka lao la kuvutia ingawa mwaka huu waliingia dosari ya kuzomewa na mashabiki wakituhumiwa kununua waamuzi lakini bado inabaki kuwa Azam ina wachezaji wenye vipaji na wanalelewa kisoka huko katika kambi ya Chamanzi.

Katika kipindi cha kwanza vijana wa Azam FC walionyesha soka hali ya juu kiasi kuwafanya viongozi wa TFF na vyama vingine vya michezo kuwa kimya na kutoamini kilichokuwa kikitokea baada ya kusikia kutoka kwa watu kuhusu kiwango cha hali ya juu cha vijana wa Coastal Union ambao mpaka kipindi cha kwanza kinaisha walikuwa nyuma kwa mabao mawili sifuri.

Hata hivyo katika kipindi cha pili Coastal Union walirudi kwa kasi na kucheza soka la hali ya juu lililoamsha kelele na kuwafanya viongozi wa soka kushindwa kukaa vitini kutokana na kiwango kilichoonyeshwa uwanjani na Coastal Union.

Mpaka dakika 90 zinaisha mabao yalikuwa 2-2, zikaongezwa dakika 30 lakini hali haikubadilika hivyo kikaja kipindi cha mikwaju ya penalt na ndipo Azam FC walipotawazwa kuwa mabingwa baada ya golikipa wao kuokoa mikwaju mitatu kutoka kwa vijana wa Coastal na kushinda kwa penalt 3-1.

Mbali ya kombe bingwa wa michuano hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Said Salim Bakhresa kupitia maji ya Uhai alipata kitita cha Tsh Milioni 1.5 wakati mshindi wa pili alipata kifuta jasho cha Tsh Milioni moja.

Kitu ambacho kinanifanya niendelee kuamini mpaka sasa kuwa Coastal Union walikuwa na kikosi bora timu yao ndiyo iliyotoa golikipa bora Mansour A. Mansour, kama hiyo haitoshi kocha wa Coastal Union Bakari Shime ndie aliekuwa kocha bora wa michuano hiyo inayofanyika kila mwaka.

Aidha Ruvu Shooting imeibuka timu yenye nidhamu, Ramadhan Mkipalamoto wa Simba ameibuka mfungaji bora kwa kufunga mabao 6 na mchezaji bora ametokea Azam FC ambae ni Joseph Kimwaga, na mwamuzi bora amekuwa ni Issck Mwalile..

Ushauri uliotolewa na Rais wa TFF kwa viongozi wa Coastal Union ni kuhakikisha wanaitunza hazina hiyo ya vipaji ambavyo kwa miaka ya baadae wanaweza kuiletea sifa Tanzania na Afrika kwa ujumla katika usakataji kabumbu.

Mafanikio ya timu hii tangu iundwe miaka mitatu iliyopita ni kushiriki mashindano manne ya vijana, mashindano ya vilabu vya Afrika mashariki na kati kwa vijana chini ya miaka 20 yaani Rolling Stone walishiriki mara mbili, ambapo mara ya kwanza waliposhiriki mwaka juzi waliishia hatua ya robo fainali mjini Arusha wakatolewa na wekundu wa msimbazi Simba.

Mashindano ya mwaka huu ya Rolling Stone yaliyofanyika mjini Bujumbura Burundi vijana wa coastal Union walipata mafanikio makubwa hata kuweza kuingia fainali wakafungwa na timu kutoka (Congo DRC), hivyo kushika nafasi ya pili.

Kombe la Uhai wameshiriki mara mbili, mara ya kwanza kushiriki walitolewa katika hatua ya makundi, baadae wakajipanga upya na mwaka huu wakaingiza tena timu kujaribu bahati. Ambao walijaaliwa kushuhudia michuano ya Uhai mwaka huu watathibitisha maneno yangu kuwa vijana walionyesha soka la hali ya juu hivyo kustahili kuingia fainali, ingawa bahati haikuwa yao.

Si vibaya maana lengo la michuano hii ya vijana si kuwa washindi kwa wakati wote, bali ni kuhakikisha soka la vijana linakuwa kwa kasi na kuihakikishia nchi wachezaji wenye uwezo na uzoefu wa kucheza soka mbele ya mashabiki wa nchi yoyote.

Si Coastal Union tu, bali timu zote zinazoshiriki ligi kuu wanatakiwa kuwalea vizuri vijana wao ili kuhakikisha maleno ya viongozi wa soka nchini yanatimia. Vijana ndiwo watakaokuja kulikomboa soka la Tanzania.
HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
+255752 593894/ +255713 593894
26/12/2012

No comments:

Post a Comment