Saturday, December 15, 2012

Tunawapiga vita lambalamba, jeshi la polisi...


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI
JESHI LA POLISI TANZANIA



  
     
 TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI TAREHE 14/12/2012

            KWA NINI LAMBALAMBA WANAPIGWA VITA DODOMA

Kwanza ni lazima tufahamu Lambalamba ni nini?
Hili ni kundi la watu ambalo wameliunda kwa lengo la kujihusisha na vitendo vya kitapeli na ulaghai kwa wananchi hususani wa vijijini, ili kujipatia mali zikiwemo fedha na mifugo ya aina mbalimbali toka kwa wanavijiji katika mkoa wetu wa Dodoma.
Kundi hili ni mkusanyiko wa watu wa jamii tofauti ambao wanatoka maeneo ya Rufiji  , Pwani, Tanga na Morogoro ambao wamekuja kuivamia jamii ya watu Dodoma ambayo nayo ina mila na desturi zake katika mambo ya jadi.
Wamekuwa wakitumia mtindo wa kujifanya kuwa wao ni waganga wa tiba za jadi kwamba wana uwezo wa kutoa vitu vya kichawi  katika majumba ya watu, sehemu za biashara  na pia kufichua  wachawi, vitu ambavyo kwa hakika hawana uwezo navyo.
Ili mtu akubalike kuwa ni mganga wa tiba za jadi ni lazima afahamike katika eneo analofanyia shughuli zake hizo kuanzia uongozi wa ngazi ya  chini hadi wa juu wa serikali na awe na kibali cha kuendesha tiba hizo kisheria kitu ambacho kundi la lamba lamba hawakidhi matakwa hayo.
Pia Mganga wa jadi kwa asili yake hatakiwi kufanya kazi zake kwa kuita baadhi ya watu ni wachawi. Hutakiwa kutoa tiba na kinga kwa kutumia miti shamba kulingana na uwezo wake, na sio wanachofanya hao wanaojiita lambalamba hii ni tofauti na sheria zinavyoelekeza.

Kwanza wanavijiji huchangishwa  na ndipo huitwa kundi hilo kuja kufanya kazi wanayodai ni ya kufichua wachawi au washirikina, ambao wanadai wanavuta mali za watu wengine kwao na kuwa matajiri.
Uchunguzi wetu umebaini kwamba wanachofanya kundi la lambalamba  kwa kushirikiana na washirika wao, huwa wanapandikiza vitu kwenye nyumba, mashamba au sehemu za biashara za mlengwa nyakati za usiku.
Baada ya kufanya hivyo ndipo wanaondoka na kundi la watu na kwenda kutoa vitu ambavyo walishavipandikiza kabla, kisha kinachotokea kwa anayefanyiwa hivyo ni kudhalilika yeye na familia yake kuwa  ni mchawi na kibaya zaidi hulazimishwa kutoa kiasi cha fedha na mifugo kama adhabu na  kutishiwa wasithubutu kwenda kutoa taarifa Polisi.
Hili ni kosa la jinai na ukiukwaji mkubwa wa haki za Binadamu, hatuwezi kuvumilia na kuwaacha wananchi wenzetu kuendelea kupoteza fedha na mali zao kwa kuwanufaisha hao matapeli.
Zipo taarifa kuwa lambalamba hao wanapofika vijijini hutafutiwa wanawake wa kuwapikia na kuwastarehesha. Huu ni unyanyasaji wa kijinsia na jambo la hatari ambalo litachangia kuenea kwa magonjwa ukiwemo UKIMWI.
Haya yanayofanyika ni utapeli mkubwa uliobuniwa na watu hao wa kujipatia fedha. Ni jambo linalodhalilisha, linalojenga chuki, na uchochezi ndani ya jamii. Pia linahatarisha usalama na  amani pamoja na afya za wanawake na jamii kwa ujumla.
Hili ni jambo la kukemea kuanzia ngazi ya Familia, Kitongoji, Mtaa, Kata hadi Taifa. Wote kwa pamoja tunaona athari zake tukemee kwa nguvu zote na wale wanaoendesha na kushabikia kundi hilo watolewe taarifa ili wakamatwe.
Watu wasiogope kutoa ushahidi dhidi ya kundi la lamba lamba na washirika wake hao wanaovuruga amani, utulivu, usalama na kurudisha maendeleo nyuma.
Tupo kwenye karne ya Sayansi na Teknolojia tusijiaibishe kwa kukumbatia mambo ya zama za kiza kwa kupumbazwa akili zetu na matapeli waliobuni mradi wa kujipatia fedha na mali kwa ujanja wa kupandikiza vitu kwenye nyumba, sehemu za biashara na mashamba, kisha baadaye wanakuja kuvitoa na kudai wamefanya hivyo kwa uwezo wao wa kubaini wachawi na kuifanya jamii yetu iishi kwa chuki na kukosa amani na kushindwa kufanya shughuli za kujiletea maendeleo   
Mwisho napenda kutoa wito kwa wananchi kwa ujumla kupitia dhana ya utii wa sheria kwa hiari kushirikiana kwa pamoja na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za watu  hao ili kuutokomeza uhalifu huu ili jamii yetu iendelee kubaki  salama na yenye amani na utulivu.


[D. A. MISIME – ACP]
KAMANDA WA POLISI [M] DODOMA

CONTACT:
POLISI MKOA WA DODOMA
DAWATI LA HABARI, ELIMU NA MAHUSIANO,
Phone:  0715 006523, Luppy Kung’alo – Mrakibu msaidizi wa Polisi (ASP)
Phone:  0712  360203, Silyvester Onesmo – Police  Konstebo  (PC)





No comments:

Post a Comment