Monday, December 31, 2012

Serikali yajipanga kukabiliana na ongezeko la watu, na kuwajali wazee na wasiojiweza.


Rais jakaya Kikwete, amewataka watanzania kufanya kazi kwa nguvu ili kuhakikisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii yanaenda sawa na ongezeko la watu nchini.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa matokeo ya sensa ya idadi ya watu na makazi katika viwanja vya mnazi mmoja jijini Dar es Salaam leo asubuhi, Kikwete amesema idadi ya watu Tanzania inaongezeka kwa asilimia 2.9 kutoka mwaka 2002 ilipofanyika sensa ya mwisho na kutoa matokeo ya watu milioni 34.4 ambapo alitabiri itakapofika mwaka 2016 idadi ya watu nchini itafikia milioni 51.

Aidha matokeo ya sensa kwa mwaka huu wa 2012 yanaonyesha Tanzania ina jumla ya watu Milioni 44,929,002 ambapo Tanzania Bara ni Milioni 43,625,434 na Tanzania Visiwani ni Milioni 1,303,568.

“Idadi hii inaonyesha dalili mbaya ambapo nchi itakuwa na mzigo mkubwa katika masuala ya kijamii na kiuchumi, idadi kubwa ya watu inamaanisha Serikali iongeze mikakati ya kimaendeleo ili kukabiliana na ongezeko hili la watu,” alisema Kikwete na kuongeza;

“Umuhimu wa kupanga uzazi uanze sasa, maana ushindani wa rasilimali chache tulizonazo utakuwa mkubwa sana miaka ya usoni, hivyo ni vema wananchi wakajulishwa umuhimu wa kupanga uzazi.”

Tangu Tanzania iundwe mwaka 1964 baada ya kuunganishwa Tanganyika na Zanzibar, hii ni sensa ya tano kufanyika ambapo sensa ya kwanza ya mwaka 1967 idadi ya watanzania ilikuwa ni milioni 12,313,54 (milioni 12.3). Tanzania bara ilikuwa na watu milioni 11,958,654 (milioni 11.9) na Tanzania visiwani kulikuwa na watu laki 3,544,00 (laki 3.5).

Hata hivyo sensa ya mwaka 2002 ilionyesha ongezeko kubwa la watu waliofikia milioni 43.625,434 (milioni 43.6) Zanzibar peke yake ilikuwa na wakaazi milioni 1.335,68 (milioni 1.3).

Katika hatua nyingine Rais Kikwete amesema haya ni matokeo ya awali ambayo yameonyesha idadi ya watu kwa ujumla. Lakini ikifika mwezi februari 2013 yatatolewa matokeo mengine yatakayoonyesha idadi ya watu kwa jinsia yaani wanawake wapo wangapi na wanaume wapo wangapi.

Mwezi Aprili 2013 yatatolewa matokeo mengine yatakayoonyesha idadi ya watu kwa umri kuanzia kata, wilaya na mikoa. Na ikifika mwezi June 2013 zitatolewa takwimu nyingine zitakazoonyesha watu wenye ajira, idadi ya kaya na masuala mingine ya kitakwimu.

Awali waziri mkuu Mizengo Pinda ambae ndie mwenyekiti wa kamati kuu ya sensa taifa amesema Serikali kwa mwaka huu imeendesha sensa kwa asilimia tisini (90%) na asilimia 10 (10%) ni wahisani, tofauti na mwaka 2002 ambapo serikali iligharamia zoezi la sensa kwa asilimia 70 (70%).

Aidha Pinda aliongeza kuwa kwa mwaka huu wataalamu wa ndani katika zoezi zima walitumika sana tofauti na mwaka 2002, ambapo kwa mwaka huu wataalamu wa kutenga maeneo ya sensa walikuwa 150, makarani 20,000 na wataalamu wengine wa takwimu 400 wote watanzania.

Pesa zilizotumika kuwalipa posho za kuendesha sensa ni milioni 90, ambapo waliweza kutoa zabuni 29 za kuendesha zoezi zima kwa kampuni za kizalendo zipatazo 29 na kuwalipa kiasi cha bilioni 11.7.

Mpaka matokeo ya awali ya sensa yanatangazwa leo serikali imetumia kiasi cha Sh bilioni 120 na kwa mujibu wa rais Kikwete ifikapo mwezi June 2013 yatakapotangazwa matokeo ya mwisho serikali itakuwa imetumia kiasi cha Sh bilioni 140 kwa zoezi zima.

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
kidojembe@gmail.com
+255 752 593894/ +255 713 593894



No comments:

Post a Comment