Tuesday, December 18, 2012

Hatimae Jenerali Ulimwengu atambuliwa rasmi kuwa wakili wa kujitegemea Tanzania...

Kutoka kushoto Jenerali Ulimwengu wa pili ni Balozi Ali Mchumo wakiwa katika shereheza 47 za kuwatambua na kuwasajili mawakili wapya katika shule ya sheria Tanzania jana.


Na Hafidh Kido

Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi gazeti la Raia Mwema Jenerali Ulimwengu, ametambuliwa rasmi kuwa wakili nchini Tanzania katika sherehe za 47 za kuwakubali na kuwasajili mawakili wapya.

Jenerali ambae kwa vipindi tofauti amewahi kuwa mkuu wa wilaya, mbunge na mwandishi wa habari amekuwa miongoni mwa mawakili wapya 618 waliokula kiapo mbele ya jaji mkuu Othman Chande katika viwanja vya Law School of Tanzania jijini Dare s salaam jana.

Akizungumza katika ghafla hiyo Jaji Chande, alisema kwa mwaka 2012 Tanzania imepata mawakili wapya 901 ingawa alieleza kwa viwango vya kimataifa ni idadi ndogo sana kwa nchi kubwa kama Tanzania.

“Mwezi July tulipata mawakili 283, na leo tumepata wengine 618 hivyo kufanya jumla ya mawakili 901 kwa mwaka huu wa 2012 kwa viwango vya kimataifa hii ni idadi ndogo sana hasa kwa nchi kubwa kama hii, tunahitaji mawakili wengi zaidi kuweza kumaliza matatizo ya kisheria yanayowakumba wananchi hasa mikoani,” alisema.

Hata hivyo jaji Chande aliongeza mbali ya idadi kubwa ya mawakili wanaopatikana kila mwaka lakini asilimia sabini (70%) ya mawakili wanaishia jijini Dar es alaam na kuacha idadi ndogo sana kuenda vijijini.

“Tanzania ina idadi ya watu wanaokaribia milioni 50, asilimia 70 ya mawakili wote wamejazana hapa Dar es Salaam, huko mikoani kuna uhaba mkubwa wa mawakili, kwa mfano Lindi kuna wakili mmoja, Kigoma wapo wawili, Sumbawanga wapo wawili, Mara wapo wanne, Njombe wapo watano, Tabora wapo sita, Tanga na Kagera wapo tisa na mikoa mipya ya Geita, Simiyu na Katavi hakuna hata wakili mmoja,” Jaji Chande.

Miongoni mwa mawakili waliosajiliwa siku hiyo ya jumatatu ni aliekuwa mwenyekiti wa umoja wa vijana CCM mkoa wa Arusha Ole Milya ambae kwa sasa amehamia chama cha demokrasia na maendeleo (chadema) amesema ataitumia elimu yake kukabiliana na migogoro ya ardhi mkoani mwake.

Sherehe hizo za kuwakubali na kuwasajili mawakili wapya zinafanyika mara mbili kwa mwaka ambapo tangu zilipoanzishwa mwaka 1986 zimefanikiwa kuzalisha mawakili wengi nchini ambao hata hivyo wameonekana kusongamana mijini na kusahau wananchi wa vijijini ambao kwa hali halisi ndiwo wanaohitaji msaada wao mkubwa hasa kutatua migogoro ya ardhi.

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
18/12/2012

No comments:

Post a Comment