Monday, December 31, 2012

Tofauti Kati Ya Mifumo Ya Analojia Na Dijitali Ya Kurusha Matangazo Ya Televisheni.

Zamil Huyu akitafakari mabadiliko ya mfumo kutoka analojia kwenda dijitali leo usiku..


Na Zamil Khalfan

Leo (tarehe 31/12/2012) ikiwa siku ya mwisho kwa nchi yetu (Tanzania) kurusha matangazo kwa njia ya analojia (analogue TV) , na kuhamia mfumo wa dijitali (digital TV), bado watu wana maswali mengi sana kuhusiana na mabadiliko haya. 

Huu mfumo mpya wa dijitali ni nini? Mfumo uliopita wa analojia ukoje? Nini tofauti kati ya mifumo hii miwili ya kurusha matangazo ya televisheni? Kwa nini tumeamua kuhamia mfumo huu mpya wa dijitali na kuacha ule wa zamani wa analojia? Makala hii itajaribu kujibu maswali hayo kwa njia rahisi yenye kueleweka, kwa hiyo endelea kusoma.

Tanzania sio nchi ya kwanza kuhamia katika mfumo wa dijitali wa kurusha matangazo ya TV. Nchi ya Uholanzi ilizima mitambo yake ya analojia mwaka 2006, na nchi kama Ujerumani, Norway, Ubelgiji, Estonia, Latvia, Hispania, Marekani na nyinginezo zilifanya mabadiliko katika kipindi cha mwaka 2009/10. Hatimaye, hatua kwa hatua nchi zote duniani zitahamia katika mfumo huu mpya, na inategemewa kwamba zote zitakuwa zimefanya hivyo kufikia mwaka 2015.


Lakini kabla ya kuuangalia huu mfumo mpya wa dijitali unavyofanya kazi na faida zake, acheni tuuangalie kwanza mfumo unaomalizika wa analojia. Tofauti kati ya mifumo hii miwili inategemea jinsi mawimbi ya matangazo ya televisheni yanavyosafirishwa kutoka kwenye vituo vya kurushia matangazo mpaka kwenye televisheni yako.

Mfumo wa analojia wa kurusha matangazo ya televisheni hauna tofauti na jinsi matangazo ya redio yanavyorushwa. Vyote vinatumia masafa ya AM na FM. Kwenye matangazo ya analojia ya televisheni, picha na video vinarushwa kupitia masafa ya AM na sauti inarushwa kupitia masafa ya FM. Njia hii ya kurusha matangazo ina kasoro nyingi kwani kiwango cha picha na sauti kinakuwa cha chini sana. Pia, mwingiliano wa mawimbi unaweza kusababisha picha au sauti kuwa na chengachenga au kutosikika vizuri hasa siku za mvamvua, au kama unaishi mbali na kituo cha kurushia matangazo. 

Pia mfumo wa NTSC wa kurusha matangazo kwa njia ya analojia haukutengenezwa kwa ajili ya kuonyesha picha za rangi. Mfumo huo ulitengenezwa baada ya vita vya pili vya dunia, wakati ambapo televisheni zilikuwa hazionyeshi picha za rangi (black and white), hivyo mpaka leo mara nyingine televisheni za analojia zinakuwa na rangi ambazo si halisi, mara nyingine hata tofauti kabisa na ile iliyorushwa na kituo cha matangazo. (kwa mfano shati ya bluu inaweza kuonekana ya njano n.k.)

Kwa upande mwingine, mfumo wa dijitali unasafirisha matangazo katika njia inayofanana na jinsi kompyuta inavyosafirisha habari. Kwa maana hiyo, TV za dijitali hazina chenga kwa sababu chenga hutokana na mwingiliano wa mawimbi ya redio. Kama upo mbali na kituo cha kurushia matangazo, picha haitaonekana kabisa.

Mfumo huu wa dijitali umetengenezwa kusafirisha picha, video, sauti na habari nyingine kwa kiwango cha juu kabisa. Pia inawezesha vituo vya televisheni kuboresha matangazo yake kwa kutia ndani sauti katika lugha zaidi ya moja, maandishi n.k katika matangazo yake. Faida nyingine kubwa ya dijitali ni uwezo wa kurusha matangazo ya HDTV (High Definition Television). HDTV ni mfumo unaoonyesha video kwa kiwango bora kabisa. 

Kwa kuwa televisheni nyingi nchini zinatumia mfumo wa analojia, kifaa kinachoitwa king’amuzi (digital to analogue decoder) kinahitajiwa ili kubadili mawimbi ya dijitali kwenda katika mfumo wa analojia ambao televisheni nyingi zinaweza kuonyesha. Pia kwa wale wanaotumia simu za mkononi zenye antenna hawataweza kupokea matangazo hayo tena, labda wawe wanatumia simu mpya zinazoweza kupokea matangazo ya dijitali, au zinazopokea matangazo kupitia intaneti. (Internet Television).

Chanzo: zamil ‘ibn kathiir’ khalfan facebook wall…

No comments:

Post a Comment