Thursday, December 6, 2012

Jamani eenhhh machakos FC wametoklezea katika gazeti la Raia Mwema la jana....


Michezo
Wanafunzi wazipaisha Kili Stars na Zbar Heroes
Kampala
Toleo la 271
5 Dec 2012
·         Huzifuata kila zichezapo
·         Kelele zao zatisha viwanjani
·         Kina Ngassa, Bocco wako juu
MICHUANO ya CECAFA inayofanyika nchini Uganda katika jiji la Kampala imefikia hatua ya nusu fainali kwa timu mbili za Tanzania kupenya hatua hiyo ikiwa ni habari njema katika timu nne kuingiza timu mbili.
Mwandishi wetu Hafidh Kido alieko Kampala anaeleza haikuwa kazi ndogo kuweza kuzichapa timu ngumu katika hatua ya robo fainali kwa Kilimanjaro Stars kuichapa Rwanda 2-0, na Zanzibar Heroes wakimaliza dakika 90 bila kufungana na Burundi iliyokuwa ikiongozwa na mchezaji aliyewahi kuchezea timu za Tanzania Suleiman Ndikumana ambaye alionekana mwiba mkali kwa golikipa wa Heroes kwa vipindi vyote viwili.
Wazanzibari hawana budi kumsifia golikipa wao Mwadini Ally ambae alifanikiwa kupangua penati kati ya mbili ambazo Burundi waliosa ikiwamo ya kwanza ya Ndikumana jumla iliyoipeleka Zanzibar nusu fainali ikiwa ni ya mikwaju 6-5.
Nia ya makala hii kuzungumzia maandalizi ya timu mbili hizi za nyumbani kushiriki michuano ya kimataifa. Imetokea bahati tu kwamba michuano hii ya CECAFA inafanyika nikiwa Kampala, na kwa bahati nzuri mji wa Kampala una Watanzania wengi ambao wanasoma na kufanya kazi, hivyo haikuwa tabu kupata washabiki wanaowapa moyo wachezaji wanapokuwa uwanjani.
Nimeona katika mitandao ya jamii na kutazama baadhi ya vyombo vya habari hasa vya Uganda na Tanzania watu wanashangazwa na kikundi kidogo ambacho kinaonekana kushangilia kwa nguvu kila timu za Tanzania zinapokuwa uwanjani.
Hiyo ni kama bahati lakini inaonekana wazi vyama cha mpira wa miguu Tanzania na Zanzibar havikujiandaa kuja na timu ya washabiki ili kuwapa moyo wachezaji. Hili ni kosa la kiufundi maana hakuna kitu kibaya kama timu kucheza ugenini bila ya kelele za mashabiki wanaowaunga mkono.
Kikundi hicho kinachosifiwa kwa kelele nyingi kila timu za Tanzania zinapocheza ni cha wanafunzi wa Watanzania wanaosoma Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Kampala (KIU), waliomua kujikusanya na kuchangishana pesa za usafiri kwenda na kurudi kila mechi.
Nilikutana na kiongozi wa kikundi hicho ambae alijitambukisha kwa jina moja la Yassin ambaye anasema: “Hakuna mtu yeyote anayetudhamini. Sisi ni Watanzania tunasoma KIU na tuna timu yetu ya Hostel inaitwa Machakos FC, hivyo tunapenda mpira na tunazipenda timu zetu za Taifa, hatuoni hasara kupoteza elfu kumi kwa siku kwenda na kurudi kila zinapocheza.”
Binafsi nimehudhuria mechi mbili tangu michuano ianze, mechi ya Kilimanjaro Stars dhidi ya Somalia iliyochezwa uwanja wa Lugogo na baadaye nikajiunga na kikundi cha Machakos FC kwenda uwanja wa Wankulukuku kuwaunga mkono Zanzibar Heroes waliokuwa wakicheza na Malawi.
Katika viwanja vyote viwili ambavyo umbali kutoka uwanja mmoja mpaka mwingine ni dakika 30, hakukuwa na mashabiki wa Tanzania. Ni Machakos FC peke yao ndio waliokuwa wakishangilia kuanzia mwanzo mpaka filimbi ya mwisho.
Hii maana yake ni kuwa kama vijana hawa wasingekuwa hapa, basi timu zetu zingecheza mwanzo mpaka mwisho wa michuano bila mashabiki. Wapenzi wa soka wanajua athari ya timu kucheza bila mashabiki.
Sikubahatika kukutana na viongozi wa TFF lakini nilionana na mbunge Juma Nkamia ambaye ni mwanahabari aliyekuwa hapa kutoa hamasa.
Alisema Nkamia kuhusu vijana hao washangiliaji wa Kitanzania: “Hakika vijana hawa wamenifurahisha sana. Mwanzo sikujua kama ni Watanzania, lakini nilipoona wamevalia fulana za timu yetu na bendera ya Tanzania nikajua ni Watanzania hivyo nimezungumza nao na pia nimewapa nauli kidogo ziwasaidie hasa baada ya kusikia ni wanafunzi.
“ Inaonyesha wana uzalendo wa hali ya juu. Maana walipotoka kule Lugogo kwenye mechi ya Kilimanjaro Stars wakaja na huku kwenye mechi ya Zanzibar Heroes. Huu ni upendo wa hali ya juu.”
Nadhani sasa kuna haja kwa vyama vyetu vya soka kuwa na mfumo wa kuviwezesha baadhi ya vikundi vya washangiliaji kwa maana ya nauli na matumizi kila timu zetu zinapocheza mechi za kimataifa ili kuwaonyesha wachezaji ya kuwa hawapo peke yao hasa kwa michuano hii inayoandaliwa ndani ya nchi za Afrika Mashariki ambako gharama za safari na kuishi bado ziko chini kidogo.
Maajabu ya Mrisho Ngasa
Mshambuliaji Mrisho Ngasa amekuwa akionyesha uwezo mkubwa hapa pamoja na nidhamu ya hali ya juu kiasi watu wanamtabiria kuwa mfungaji bora na hata kuwa mchezaji bora wa michuno hii.
Ni maajabu kwa mchezaji kuwa mwenye magoli mengi katika mechi moja tu, Ngasa hakufanikiwa kufunga goli hata moja katika mechi mbili za mwanzo dhidi ya Sudan na Burundi, lakini akaushangaza umma wa Waganda na wageni waliopo hapa baada ya kufunga magoli matano peke yake siku Kilimanjaro Stars ilipoinyuka Somalia kwa mabao 7-0. Kati ya magoli hayo ya Ngassa, la kwanza lilikuwa goli la mapema zaidi katika michuano hii akiwa amelipachika katika sekunde ya 47 ya mchezo.
Siku hiyo magoli mengine mawili yalifungwa na John Bocco ambaye naye yumo katika orodha ya wafungaji bora akiwa na magoli matano, goli moja akiwa amefunga dhidi Rwanda juzi Jumatatu.
CECAFA kushindwa kujipanga
Waswahili wanasema kila masika hayakosi mbu, Chama cha Soka cha Uganda (FUFA) ambao ni wenyeji wa michuano hii kimebabaika baada ya uwanja walioutegemea wa Namboole kujaa maji kiasi mechi kuhamishiwa katika viwanja ambavyo havina hadhi ya michuano hiyo mikubwa katika nchi za Afrika Mashariki.
Awali michuano hii ilitakiwa kuchezwa katika viwanja viwili vya mjini Kampala; Nakivubo kilicho katikati ya mji pembeni ya Soko la Owino, na uwanja mkubwa wenye hadhi ya kimataifa Namboole ambao unajulikana kama Mandela Stadium kwakuwa ulijengwa kwa msaada kutoka kwa Rais wa zamani wa Afrika Kusini Nelson Mandela.
Lakini mpaka michuano inaanza ni Namboole tu uliokuwa tayari kwa michuano hiyo baada ya Nakivubo unaomilikiwa na Jiji la Kampala (KCC) kushindwa kuwa tayari kwa michuano, hivyo FUFA wakaamua kupendekeza uwanja wa Lugogo ambao nao upo chini ya (KCC) ambao hadhi yake ni kama uwanja wa Azam Chamazi. Hivyo kuwa na viwanja viwili Namboole na Lugogo.
Hata hivyo baada ya Namboole kujaa maji ikabidi kipendekezwe kiwanja kingine cha Wankulukuku kilichopo karibu na kilima cha Mengo njia ya kuelekea Masaka, mashariki mwa Uganda. Kwa hakika kiwanja hicho ni cha hadhi ya chini. Kimetumika tu kwa kuwa ni lazima kitumike.
Katika hatua nyingine, taarifa zilizopamba magazeti ya Jumanne zilikuwa ni za kusimamishwa kazi kwa Mwenyekiti wa Bodi ya Uwanja wa Nakivubo, Geoffrey Kisseka, akidaiwa na Waziri wa Michezo wa Uganda, Charles Bakkabulindi, ya kuwa ameshindwa kuitisha mkutano wa Bodi kwa muda mrefu na kushindwa kuuandaa uwanja kwa ajili ya michuano ya CECAFA hali iliyofanya nchi kupata aibu kubwa.
Hakuna marefu yasiyo na ncha, michuano hii inatarajiwa kukamilika Jumamosi hii huku nusu fainali zikipigwa kesho Alhamisi.
Fainali itachezwa kwenye Uwanja wa Namboole kuhitimisha michuano hiyo iliyosisimua na kuonyesha vipaji vya hali ya juu kwa timu washiriki ambazo ni Tanzania Bara, Zanzibar, Kenya, Uganda, Burundi, Sudan, Sudan ya Kusini (ambayo inashiriki kwa mara ya kwanza), Eritrea, Ethiopia, Somalia, na Malawi ambayo ni timu mwaalikwa.
Mpaka sasa wafungaji wanaoongoza ni Mrisho Ngasa (5, Kilimanjaro Stars), John Bocco( 5, Tanzania), Umony (3, Uganda), Ndikumana (3, Burundi), Nduwagira (3, Burundi) na Msowoya (3, Malawi).

Soma zaidi kuhusu:

Tufuatilie mtandaoni:


No comments:

Post a Comment