Friday, December 21, 2012

Sakata la makamu mwenyekiti taifa Chadema kutupa kadi ya uanachama kikaoni....


KATIBU mkuu wa Chadema, Dk Willbroad Slaa amesema chama hicho kinasubiri kupokea taarifa ya mgogoro unaofukuta ndani ya chama hicho mkoani Katavi na kusababisha Makamu Mwenyekiti wake Taifa , Said Arfi, kutupa kadi yake ya uanachama.

Ameeleza kuwa Katiba ya chama hicho inaeleza wazi kwamba unapoibuka mgogoro, unatakiwa kuripotiwa katika ofisi ya Katibu Mkuu Taifa ndani ya siku 14. Tukio la Arfi kutupa kadi ya Chadema lilikuwa la pili ndani ya wiki moja, kwani juma lililopita uliibuka mgogoro mwingine wilayani Karatu ambako pamoja na mambo mengine uliishia kwa Kamati Kuu kuusimamisha uongozi wote wa chama hicho wilaya.

Arfi ambaye ni Mbunge wa Mpanda Mjini, alitishia kujitoa Chadema juzi, katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya chama hicho Mikoa ya Katavi na Rukwa kilichoketi Namanyere, Nkasi na kufikia uamuzi wa kumsimamisha Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Mkoa wa Rukwa, Laurent Mangweshi.

Katika kikao hicho, Arfi anadaiwa kuichukua kadi yake ya Chadema na kumtupia Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Rukwa, John Mallack akitangaza kuachia nyadhifa zote alizonazo, kisha kuondoka ukumbini, kabla ya kufuatwa na wazee wa chama hicho na kumsihi aichukue kadi yake hiyo.

Hata hivyo, Mangweshi jana aliliambia Mwananchi kwamba hajapewa barua hiyo mpaka sasa na kwamba yeye bado ni Mwenyekiti wa Bavicha mkoa wa Rukwa, kauli ambayo ilipingwa na Katibu wa chama hicho mkoani Rukwa na Katavi, Ozem Chapita aliyesema kuwa ipo tayari na wameisafirisha kwa basi jana mchana ili imfikie.

Akizungumzia tukio hilo jana Dk Slaa alisema  taarifa hizo amezisikia ila hawezi kutoa maamuzi kwa kuwa Chadema kinafuata taratibu za vikao pamoja na Katiba yake.

“Utaratibu wa chama ni kwamba malalamiko yeyote ni lazima yawasilishwe katika ofisi ya Katibu Mkuu ndani ya siku 14” alisema Dk Slaa na kuongeza; “Mimi kama Katibu Mkuu ni lazima nifuate taratibu za chama na sio kufanya vinginevyo.” Alisema kuwa taarifa hizo amezisikia kupitia vyombo vya habari na kwamba anachokisubiri ni taarifa rasmi ya maandishi ili kama chama kiweze kukaa vikao na kujadili mgogoro huo.

Alipoulizwa kuna taarifa kwamba baadhi ya makada wa chama hicho wanatumiwa kukivuruga, Dk Slaa alisema kuwa inawezekana hilo likawa na ukweli lakini kama kawaida ya chama hicho, hakitoi maamuzi bila ya kukaa vikao.

“Hizo ni taarifa ambazo zipo na zinaandikwa kila siku katika vyombo vya habari, zikija rasmi katika ofisi ya chama zitajadiliwa” alisema Dk Slaa.

Arfi alifikia hatua hiyo baada ya kutokea sintofahamu kati ya wajumbe wa kikao hicho katika uamuzi huo uliofikiwa kwa kupiga kura za ndiyo na hapana.


Vyanzo vya habari kutoka ndani ya kikao hicho vilifafanua kuwa Arfi alikerwa na kauli iliyotolewa na Mangweshi kuwa katika Uchaguzi Mkuu uliopita, alipokea rushwa kutoka kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Vyanzo hivyo vya habari vimeeleza kuwa kutokana na hali hiyo, Arfi alipandwa na hasira na kuamua kumrushia kadi Mallack kisha kutoka nje ya ukumbi. “Hatua hiyo ilifanya wajumbe wa kikao hicho nao kutoka nje ya ukumbi na kuanza kumbembeleza ili asichukue uamuzi huo na kisha wakamwekea kadi yake ya uanachama katika mfuko wake wa shati,” alisema mmoja wa makada hao.Arfi mwenyewe hakupatikana juzi kuzungumzia tukio hilo na hata jana alipotafutwa simu zake zote zilikuwa zimezimwa.


Imeandaliwa Fidelis Butahe, Dar na Juddy Ngonyani, Katavi, Burhani Yakub, Tanga na Mussa Juma, Arusha

Chanzo: http://www.mwananchi.co.tz/habari

No comments:

Post a Comment