Thursday, March 28, 2013

Kifo cha Mbunge wa Chambani chaacha huzuni kubwa, Rais Kikwete atoa ndege ya Rais kusafirishia maiti kuelekea Pemba.


Mbunge wa Chambani (CUF),marehemu Salim Hemed Khamis akiwa amebebwa na baadhi ya wabunge na watumishi wa Bunge baada ya kuanguka ghafla wakati akihudhuria vikao vya kamati za Bunge juzi.Picha na Nuzulack Dausen.  

Mbunge wa Chambani (CUF), Salim Hemed Khamis (60) amefariki dunia jana katika hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) alikokuwa amelazwa baada ya kuanguka ghafla juzi kwenye Ofisi za Bunge, Dar es Salaam.
Kifo cha mbunge huyo kimewagusa wengi akiwamo Rais Jakaya Kikwete ambaye ametoa ndege yake ili kusafirisha mwili wa marehemu kwenda Pemba. Ofisi ya Bunge imethibitisha kutokea kwa kifo hicho cha mbunge huyo na kueleza kuwa, alipatwa na ugonjwa wa kiharusi uliosababishwa na ugonjwa wa moyo (Hypertension).

Khamis anatarajiwa kusafirishwa kisha kuzikwa leo kijijini kwao Chambani, Pemba baada ya jitihada za kumsafirisha jana kushindikana na wabunge wengi kuomba kushiriki kumuaga.
Mbunge huyo atasafirishwa leo saa tatu asubuhi baada ya shughuli ya kuaga itakayofanyika kwenye Viwanja vya Ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam. Spika wa Bunge, Anne Makinda ametangaza kusitishwa kwa shughuli zote za Kamati za Bunge hadi Jumanne Aprili 2, kutokana na msiba huo.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Makinda alisema: “Ninatoa pole kwa familia ya marehemu, wananchi wa Chambani, Wajumbe wa Kamati ya Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa, wabunge wote na Watanzania wote kwa jumla”.

Khamis alianguka juzi saa 10.50 asubuhi wakati akishiriki kwenye kikao cha Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kilichofanyika katika ofisi za Bunge jijini Dar es Salaam.

Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel alisema wamepokea taarifa za kifo hicho kwa masikitiko ambacho kilisababishwa na kupasuka kwa mshipa wa damu kichwani.

“Tumeelezwa na daktari kuwa Mbunge Salim amefariki kutokana na kupasuka kwa mishipa ya damu ambayo ilimiminikia kwenye ubongo wake na kuenea kichwani,” alisema Joel. Alisema kutokana na hali hiyo shughuli zote za uchambuzi wa bajeti zilizokuwa zikifanywa na kamati za Bunge, zimeahirishwa kwa mujibu wa taratibu zilizopo hadi tutakapomaliza shughuli za mazishi.

Joel alisema kwa upande wa Bunge, shughuli za msiba zitaongozwa na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ambayo marehemu alikuwa mjumbe.

Alisema Bunge linamshukuru Rais Kikwete kwa kutoa ndege yake kwa ajili ya kupeleka mwili huo Pemba na kwamba hatua hiyo itatoa fursa kwa wabunge wengi kushiriki mazishi.
Alisema kutokana na hali hiyo wabunge 12 wakiongozwa na Lowassa watakwenda kushiriki kwenye msiba.

Wabunge, CUF waomboleza
Baadhi ya wabunge jana walionekana kuchanganyikiwa baada ya kupata taarifa za msiba huo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti walisema kuwa kifo hicho ni cha ghafla kwa sababu Salim alikuwa kwenye vikao vya Bunge tangu walipoanza vikao vya kamati.

“Tangu tuanze vikao vya kamati tulikuwa naye na alionekana kuwa mwenye afya, kwangu mimi ni pigo nimepata kwa sababu alikuwa mwalimu kisiasa katika Chama cha CUF,” alisema Rajab Mohamed Khamis, ambaye ni Mbunge wa Ole (CUF).

Kwa upande wake, Mbunge wa Peramiho CCM, Jenister Mhagama alishtuka na kuonekana kutoamini taarifa hizo, jambo ambalo lilimfanya ashindwe kuzungumza chochote.
Wabunge wengi walionekana wakihaha kutafuta usafiri ili wawezekwenda Muhimbili huku baadhi yao wakienda kujiandaa na safari ya kwenda Pemba.
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro alisema chama chake kimepata pigo kubwa kutokana na kifo cha Mbunge, ambaye amemwelezea kwamba alikuwa nguzo muhimu kwa chama hicho.

Mtatiro alisema marehemu alikuwa na mchango mkubwa kwa chama chake kutokana na shughuli mbalimbali alizokuwa akizifanya katika chama hicho.

Alisema kuwa marehemu ndiyo alikuwa Mnadhimu Mkuu wa Wabunge wa CUF, pia alikuwa Mkurugenzi wa Uchaguzi wa chama hicho kuanzia mwaka 2010 hadi 2012.
“Pia alikuwa anatusaidia sana wakati tukiwa na migogoro kwani kutokana na busara zake alikuwa anaheshimika sana,” aliongeza Mtatiro.

Kuumwa kwake
Alianza kujisikia vibaya akiwa kwenye kikao cha kamati juzi na alianguka hivyo wabunge wenzake kwa kushirikiana na Ofisi ya Bunge walimchukua na kumpeleka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya matibabu.

Alilazwa kwenye chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu, hadi alipokutwa na mauti jana.

Miezi mitatu iliyopita alikuwa nchini India katika Hospitali ya Apollo kwa ajili ya matibabu na alirejea nchini na kuendelea kushiriki shughuli za Bunge na za chama chake.

Hoja ya mwisho kuchangia katika vikao vya kamati ni ile ya Machi 26, mwaka huu, pale alipoukosoa Mpango wa Afrika Kujitathmini Kiutawala Bora (APRM) kwa kushindwa kutoa taarifa za kweli kuhusu rushwa kwenye taasisi nyeti zikiwemo polisi, magereza na hospitali.

Rekodi Bungeni
Khamis aliingia bungeni kwa mara ya kwanza 2005 na kuchaguliwa tena 2010. Katika Bunge la 10 aliuliza maswali ya msingi matano, ya nyongeza saba na alichangia hoja mbalimbali mara 18.

Historia yake
Mbunge huyo, ambaye alizaliwa mwaka 1952, alisoma Shule ya Msingi Pandani kati ya 1959 na 1960 na kumalizia katika Shule ya Msingi Kengeja kati ya 1960 na 1967.
Elimu ya sekondari aliipata kati ya 1968 mpaka 1969 katika Shule ya Chambani na kuhamia Shule ya Fidel Castro aliposoma kati ya 1970 mpaka 1971. Kati ya 1972 hadi 1973 alikuwa katika Chuo cha Lumumba kwa shahada yake ya kwanza ya Kilimo.

Alisoma shahada yake ya uzamili katika Chuo cha Commonwealth Mycological cha Uingereza kati ya 1988 hadi 1989.

Kabla ya kuwa mbunge alifanya kazi sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwa Mwalimu kati ya 1974 mpaka 1978, huku 1984 mpaka 1996 akifanya kazi katika Kampuni ya Mohamed Sugar.

1997 alijiunga na Kampuni ya SAS Ltd alipofanya kazi mpaka 2001 kabla ya kupata Ubunge 2005 hadi mauti ulipomkuta.
Salim ni mbunge wa kwanza kufariki kwa mwaka huu, ingawa katika Bunge hili anakuwa Mbunge wa nne.

Wabunge wengine waliofariki ni Mussa Khamisi Silima wa Zanzibar, Mbunge wa Viti Maalumu wa Chadema Regia Mtema pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki, Jeremia Sumari.

Chanzo: Gazeti Mwananchi.



No comments:

Post a Comment