Thursday, March 7, 2013

Waya wa umeme wenye thamani ya 300mil ulitaka kuuzwa kwa 2.5mil...


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Iddi, akiangalia waya wa umeme aina ya shaba ambao amezuia mauzo yake hadi uongozi wa kiwanda cha sukari utapokaa pamoja na Wizara ya fedha kufikia maamuzi, kutokana na waya huo kuuzwa chini ya thamani na baadhi ya maafisa wa Serikali. Thamani halisi ya waya huo inakadiriwa kuwa ni Tsh300Millioni lakini umeuzwa kwa Tsh.2.5Millioni tu.

KATIKA hali isiyo ya kawaida waya wenye thamani ya zaidi ya Tsh300Millioni mali ya Serikali ya mapinduzi Zanzibar umeuzwa kwa Tsh.2.5Millioni na baadhi ya maafisa wa serikali hiyo hali iliyosababisha makamu wa pili wa Rais Zanzibar kuzuia uuzwaji wa waya huo na kampuni iliyonunua.

 Tukio hilo limebainika mara baada ya Makamu huyo kutembelea kwenye kiwanda Cha Sukari kilichopo Mahonda mjini Zanzibar na kuzungumza na uongozi wa kiwanda hicho, ambacho kiliuziwa waya huo kwa bei chee.
  Balozi Seif alisema zipo hitilafu zinazotumiwa na baadhi ya maafisa wa Serikali katika mauzo ya mali za Serikali na matokeo yake kusababisha kuitia hasara kubwa Serikali Kuu.
  Amesema Mali za Serikali zimekuwa zikinunuliwa kwa gharama kubwa lakini uuzwaji wake baada ya matumizi hayalingani na thamani ya mali zenyewe jambo ambalo hutoa mwanya kwa mali hizo kuuzwa kwa bei ya chini kabisa.
 “ Utashangaa kuona mali za Serikali hununuliwa kwa gharama kubwa lakini baadhi ya maafisa na watendaji wa serikali hutumia mwanya wa kujenga hoja ya kuuzwa mali hizo kwa kisingizio cha kuchakaa na badala yake baadhi yao kujiuzia wenyewe kwa bei wanayoitaka wao wenyewe bila ya kuzingatia taratibu zilizopo za tenda na mnada”. Alionya Balozi Seif.
  Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliuagiza Uongozi wa Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo kukaa pamoja na Uongozi wa Kiwanda cha Sukari kuangalia nanma ya     matumizi ya waya huo ambao ulikuwa ukitumiwa na Kiwanda hicho.
  Waya huo ulilazimika kufukuliwa na Uongozi wa Kiwanda hicho baada ya kubainika kuanza kuhujumiwa kwa kukatwa katwa na baadhi ya wezi kufuatia kutambulikana thamani yake katika masoko ya Kimataifa.   
Mapema Mshauri wa Kiwanda cha Sukari Mahonda  Dr. Hamza Hussein Sabri alisema Zanzibar inatarajiwa kujitosheleza kwa Sukari ifikapo mwishoni mwa mwezi Oktoba mwaka huu kufuatia uongozi wa Kiwanda cha sukari Mahonda kufanikiwa kupata washirika zaidi katika kuongeza nguvu ya kuanza uzalishaji wa bidhaa hiyo muhimu kwa matumizi ya Jamii.

Chanzo: Saidpowa blog.



No comments:

Post a Comment