Friday, March 8, 2013

Siku ya wanawake duniani inamaanisha kitu kimoja tu kwangu, ushupavu.

Rais wa Liberia Ellen Johnson Sirleaf, ni mfano bora wa mwanamke wa chuma na msomi wa hali ya juu.




Leo tarehe 8 March, wanawake duniani wanasherehekea siku yao. Mpaka sasa sijajua wanasherehekea siku yao kwa namna gani. Kupata uhuru, haki ama usawa.

Lakini kwa namna jambo hili lilivyowekwa inaonyesha wanawake wanakata minyororo ya udhalilishwaji na unyonge kutoka kwa wanaume ama mfumo dume ambao ‘unampendelea mwanaume’ kuwa mmiliki wa dunia.

Mungu anasema mwanamme ni kiongozi kwa mwanamke; na hata wanandoa siku yao ya harusi huambiwa na viongozi wa dini na kijamii kuwa mume amlinde mke kwa maisha yake yote.

Na hata katika utengano mume ndie anaeamua kuachana na mke. Lakini jamii zilizoendelea hasa nchi za magharibi mtu yeyote anaweza kuamua mustakabali wa ndoa. Mume ama mke anaweza kusema inatosha, kila mmoja ashike njia yake. Ila nchi za kiafrika na Asia bado mustakabali wa ndoa upo mikononi mwa mume.

Sitaki kushindana na mvumo wa mabadiliko wa kudai usawa. Lakini mpaka sasa kuna kazi ambazo mwanaume hawezi kuzifanya kama ambavyo mwanamke kuna kazi hamudu kuzifanya bila msaada wa mwanamme.

Zamani ukiona mwanamke anaendesha gari hiyo ni ajabu akidi; lakini sasa ni jambo la kawaida sana kumuona mwanammke anaendesha gari. Ingawa kuna aina ya magari, hata imezoeleka magari yenye maumbo madogo yananasibishwa na jinsia ya kike. Si ukariri wa mambo lakini maumbile ndivyo yanayoisukuma akili kuamini hivyo.

Tukubali kutokubaliana kuwa mwanamke na mwanamme katu hawawezi kuwa sawa. Udhaifu unaanza pale mwanamke anapolazimisha kupata haki ama usawa huo.

Usawa haudaiwi, huwezi kudai usawa bali maumbile ndiyo yanayoamua hivyo. Ikiwa unaamini aina fulani ya shughuli inaweza kufanywa na jinsia zote basi haina haja kuutangazia umma hivyo. Bali njia rahisi ni kutumbukia na kuifanya.

Ukelele wa mabadiliko hauna maana ikiwa unatawaliwa na dhana; kinachopasa kufanywa ni vitendo na si maneno. Hujisikia uchungu sana kusikia wanawake wanalalamika kuwa hawatendewi haki katika jamii.

Dhamira ya dhati ndiyo inayoamua usawa, mwanamke amua sasa kupambana. Kelele haziwezi kuwafikisha popote zaidi ya kuendelea kuwaona wasumbufu.

Siku ya wanawake duniani haifai kutumika kudai haki za wanawake bali itumike kujipongeza kwa kuumbwa wanawake. Mwanamke ni mtu bora sana katika dunia hakuna mfano wake.

Mama ndie anaezaa kila kiumbe. Mtoto anaweza kuzaliwa bila baba lakini katika historia dunia tangu imeanzishwa hakuna kiumbe aliekuja katika dunia hii bila mama.

Waamini wa dini watakubaliana nami kuwa Adam na Hawa ndiwo viumbe pekee wa ajabu ambao wameumbwa kimaajabu. Baba yetu Adam aliumbwa kwa mikono mitakatifu ya Mungu, hakuwa na baba wala mama.

Mama yetu Hawa alitoka ubavuni mwa Baba yetu Adam hivyo bibi Hawa amekuja duniani bila mama, na Adam hawezi kuwa baba yake maana baadae alimuoa. Mungu alitaka tu kuonyesha uwezo wake.

Lakini yote haya yalitokea mbinguni, na si hapa duniani. Kioja kilichowahi kutokea duniani ni kimoja tu cha kuzaliwa Nabii wa Mungu Issa ama Yesu na mama pekee bila baba.

Hadithi hii inaonyesha utukufu wa mwanamke, maana mama ndie anaweza kulea mtoto, kumlisha na kumpa raha zote za mwanzo katika dunia.

Hata Mtume wa Waislamu Mohammed (SAW), wakati anazaliwa baba yake alikuwa ameshaaga dunia. Funzo hili linaonyesha kuwa mtoto hawezi kuzaliwa mama akiwa amekufa, ila mtoto anaweza kuzaliwa baba akiwa amekufa. Utukufu ulioje huu wa mwanamke.

Kitu kingine cha kuonyesha utukufu wa mwanamke katika jamii ni namna mama anavyopewa hadhi mbele ya mtoto wake, maana mtoto anaweza kuitwa wa haramu akizaliwa nje ya ndoa, na kwa upande wa Waislamu mtoto wa aina hiyo hafai kurithi ama kurithiwa na baba aliemzaa bila kumuoa mama yake. Lakini mama anakuwa na haki zote kwa mtoto huyo, wanawake wanataka nini tena mbele za Mungu mtukufu?.

Makala haya yana lengo moja tu, kumfanya mwanamke kujiamini na kuon ana bahati kubwa sana katika jamii. Mwanamme hawezi kukamilika bila ya kuoa. Heshima ya mwanamme inaongezeka baada ya kuoa.

Na katika kila mafanikio ya mwanamme basi nyuma yake kuna mwanamke mwema aliemshauri. Anaweza kuwa mama ama mke wake. Na hata katika maisha mke na mama ndiwo watu wanaouma sana kuwakosa.

Fanya utafiti katika maneno haya na utaamini hakuna haja ya kuwa na siku ya wanawake. Bali wanawake kila siku ni siku yao ya kujiamini na kujipongeza kwa utukufu walio nao.

HAFIDH KIDO
8 March, 2013
Dar es Salaam, Tanzania

No comments:

Post a Comment