Monday, March 11, 2013

Kibanda kufanyiwa upasuaji bila kisu....



.
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda amefanyiwa upasuaji wa kitaalamu bila kutumia kisu na madaktari wanaomtibu katika Hospitali ya Milpark, Johannesburg, Afrika Kusini.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Katibu Mkuu wa TEF, Neville Meena katika operesheni hiyo iliyofanyika juzi saa 5.30 asubuhi, walipitisha mipira kwenye matundu ya pua  na kutibu matatizo yaliyokuwa yakimkabili ndani ya mwili wake.
Taarifa hiyo ilisema madaktari walichukua hatua hiyo ili kuepuka kumwongezea majeraha zaidi mhariri huyo mtendaji wa New Habari (2006), ambaye alikuwa na vidonda kutokana na kukatwakatwa na wavamizi.
Upasuaji aliofanyiwa ni pamoja na ule wa kuondoa jicho la kushoto, pia kurekebisha taya lake la kushoto.
Taya hilo na meno ambavyo vilibainika kupata mtikisiko vimefungwa waya maalumu ili kuvirejesha katika hali ya kawaida.
Kuhusu jicho lililong’olewa, madaktari wamepanga kumwekea jicho la bandia ambalo hata hivyo, halitamwezesha kuona.
“Jicho hilo linasubiri uamuzi wa madaktari wanaomtibu ambao wamesema wanasubiri kupona kwa jeraha alilopata,” iliongeza taarifa hiyo.
Meena alisema katika taarifa hiyo kuwa Kibanda alikuwa na nafuu kubwa jana kuliko ilivyokuwa siku za mwanzo.
Alisema madaktari walimweleza kuwa sura yake ilikuwa imeanza kurejea katika hali ya kawaida na uvimbe wa damu umepungua.
“Tunamshukuru Mungu kwamba mwenyekiti wetu anaendelea vizuri baada ya upasuaji wa saa 05.30 uliofanyika jana Jumamosi. Anazungumza vizuri kiasi cha kuwatia matumaini wanaomuuguza,” alisema Meena katika taarifa hiyo na kuongeza kuwa anaendelea kutumia dawa akiwa chini ya uangalizi wa madaktari na wauguzi.
Milpark anakotibiwa Kibanda ni moja ya hospitali bora barani Afrika ambayo hata Rais mstaafu wa Afrika Kusini Nelson Mandela hutibiwa hapo.
Chanzo: Gazeti Mwananchi.

No comments:

Post a Comment