Wednesday, March 20, 2013

polisi wazidi kuwahoji waliosababisha kifo cha Traffic msafara wa Rais.


Dar es Salaam. Dereva wa gari lililomgonga na kumuua askari wa usalama barabarani, Elikiza Nko (pichani)  atafikishwa kortini wakati wowote baada ya upelelezi kukamilika, ilielezwa jana.
Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini(trafiki), Mohammed Mpinga alisema hayo jana alipozungumzia tukio hilo ambalo lilisababisha simanzi kwa watu wengi.
Mpinga alisema polisi walifanikiwa kumkamata mhusika kwa mbinu za kipolisi na kwamba kwa jana alikuwa akihojiwa ili kupata ushahidi utakaowezesha kumpeleka kortini.
Alisema dereva huyo ni kati ya wale wawili waliowakamata   awali na  hatimaye mmoja walimbaini kuwa ni mhusika .
‘’Juzi usiku tuliwahoji na mmoja wao alitudanganya, tulipomuuliza dereva wa gari hili ni nani akajibu siyo mimi nimeachiwa na mwenyewe amekimbia” alisema Kamanda Mpinga na kuongeza kuwa baada ya kumbana alikiri kuwa ndiye.
Kwa mujibu wa Kamanda Mpinga marehemu ameacha mume na watoto watatu. Maziko yanatarajiwa kufanyika leo katika makaburi ya Mbweni yaliyopo Manispaa ya Kinondoni na yatahudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa.
Marehemu alifariki dunia baada ya kugongwa na gari lililokurupuka kuufuata msafara wa Rais Jakaya Kikwete eneo la Bamaga Mwenge jijini Dar es Salaam Jumatatu iliyopita alipokuwa katika ziara ya kutembelea mkoa huo.
Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment