Sunday, March 17, 2013

Ridhiwani Kikwete alia na watu walioingia kwenye ukurasa wake wa facebook 'hackers' na kuandika habari mbaya.


Ndugu zangu,
Habari za mapumziko ya mwisho wa wiki. Yapo mambo machache ningependa kuwashirikisha ili kuweka kumbukumbu sawa, na pia kuzuia upotoshaji ambao unaweza kujitokeza siku za usoni iwe kwangu, kwako au kwa mtu mwingine.

Mojawapo ya mambo makubwa ambayo yamejitokeza siku za karibuni hasa katika suala la Teknolojia na habari ni jambo la sheria za faragha (privacy and privacy laws). Tumeshuhudia kufungwa kwa gazeti za News of The World mali ya bilionea Rupert Murdoch wa Kimarekani baada ya kudhihirika alitumia wataalam wa teknolojia (hackers) kutafuta siri za watu mashuhuri kwa kuingia katika simu zao za mkononi kinyume cha utaratibu na sheria za faragha (Privacy Laws). Tumeshuhudia pia wahalifu hao hao wa mtandao wakifanya mengi kama kuvamia kwa mitandao ya makampuni makubwa kama Sony na mengineyo na hata katika mitandao hii ya kijamii upo wakati marafiki zako wanakwambia mbona umenitumia kitu kisichoeleweka, na baadaye kuja kugundua kwamba si wewe uliyefanya hivyo.

Tarehe 1, 8 na 9 mwezi huu wa Machi nilikuwa Dar es Salaam kwa shughuli zangu za kawaida kimaisha lakini ziko updates 5 zilifanyika hapa moja ikimhusu ndugu Absalom Kibanda. Ni ajabu kwamba baadhi ya waandishi tena waliojivika taji la usahihi katika uandishi waliiandika habari hiyo bila hata kuniuliza kwamba ni nini kinatokea. Tunajitahitahidi na kutamani kuwa na Taifa la waandishi makini na wenye kufuata maadili lakini wapo wanaoturudisha nyuma. Ni ajabu gazeti kuandika jambo lisilo la kweli huku wahusika wakiwa na kila uwezo wa kumfikia yule wanayedhani kwamba ameandika na kumhoji ili kuhakiki habari. Kazi ya uhariri ni kuhakiki. Ikiwa mtu atakimbilia kuandika jambo likuhusulo ambalo hana hakika nalo na alikuwa na kila uwezo wa kuwasiliana na wewe na kukuuliza lazima utajiuliza maswali mengi. Kwanza, nini hasa lengo lake? Pili, ufahamu wake wa kile anachokifanya kwa maana ya taaluma yake katika kazi anayoifanya.

Napenda kuwaambia kwamba katika tarehe hizo mwezi huu wa Machi, wahalifu wa mtandao wakiwa eneo la Njiro na baadaye Kijenge mjini Arusha, kila post ilionyesha eneo ilipotoka, (wakati huo mimi nikiwa Dar es Salaam) waliingia bila idhini kwa njia haramu (Hacking) katika anuani yangu ya Facebook na ku-post habari hizo tano. Sasa nimeliacha jambo hilo katika vyombo stahiki vya ulinzi na usalama ili kufuatiliwa kadiri ya taratibu zao.

Natoa wito kwa ndugu zangu waandishi kujitahidi kuhakiki habari kabla ya kuzipeleka katika vyombo vyao na pia wahariri kuzingatia kuhakiki habari kabla ya kuzichapisha hasa kama chombo chako cha habari si cha habari za udaku. Hii itasaidia wao kujenga heshima mbele ya jamii, kufikisha kile hasa ambacho ni habari na kuzuia mikanganganyiko isiyo ya lazima. Haya yakizingatiwa nadhani hata sintofahamu hizi za uandishi wa habari unaotokana na hisia na vyanzo vumbi na ufahamu mdogo wa jambo utaondoka na tutakuwa na jamii ambayo haki na uwajibikikaji wa wanahabari kwa jamii utaonekana kutendeka.

Niombe radhi kwa ndugu yangu, rafiki yangu na pia mwalimu wangu, Ndugu Absalom Kibanda kwa usumbufu wowote uliojitokeza ambao naamini watu wasio na nia njema walitaka kuutumia kuleta hisia tofauti katika jamii na pia kumpa pole kwa mara nyingine tena kwa maumivu yaliyosababishwa na ujangili huo. Namuombea kwa Mungu ampe unafuu mapema zaidi ili arudi katika meza yake kuendeleze harakati za kupambana na mchango wake katika kuleta maendeleo ya kweli kwa nchi yetu. Nawapa pole pia wale wote ambao kwa namna moja au nyingine walikwazwa na uzushi huo, kwa kuwa sina tatizo lolote na Ndugu Kibanda na wala nisingependa lililomtokea limtokee yeye wala mtu mwingine yeyote.

Ni imani yangu ya dhati kwamba vyombo husika katika nchi yetu havitasita kulitalifanyia kazi jambo hili na ukweli juu ya nini kimemtokea Bwana Absalom Kibanda utajulikana na kuwekwa bayana.

Mwisho, shukrani kwa wote mlionipigia simu kuhusu hili, tuko pamoja na nawatakia kila la kheri katika shughuli za ujenzi wa Taifa letu hili la Tanzania ambalo msingi wake umejengwa katika haki, umoja, amani na kujali hali za watu wake.

Asanteni sana.

Ndugu yenu,
Ridhiwani Kikwete,
Dar es Salaam, Jumapili Machi 17, 2013.

No comments:

Post a Comment