Monday, March 11, 2013

Wamiliki wa vyombo vya habari waanza kusema Mitambo ya digital inawatia hasara.



Dar es Salaam. Wamiliki wa vituo vya utangazaji vya televisheni nchini, wamesema watasitisha kurusha matangazo ndani ya mwezi mmoja kuanzia sasa kutokana na kushindwa kumudu gharama za uendeshaji.

Hatua hiyo inatokana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuzima mitambo ya analojia na kuhamia dijitali Desemba 31, mwaka jana kitendo walichodai kimepunguza mapato yanayotokana na matangazo.

Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania (Moat), Reginald Mengi alisema hakuna haja ya kurusha matangazo kwa hasara.
Mengi alisema kutokana na kuanza kwa mfumo wa dijitali, watangazaji wamesitisha kutoa matangazo kwa sababu wananchi wengi hawana ving’amuzi.

Kama mamlaka itashindwa kurudisha ule mfumo wa analojia kuwa sambamba na dijitali hadi wananchi watakapokuwa na ving’amuzi, tutazima televisheni zetu ndani ya mwezi mmoja ujao,” alisema Mengi.

“Ibara ya 18 ya Katiba imekiukwa kutokana na wananchi kunyimwa fursa ya kupata habari, hivyo hali hii hatutaki iendelee,” alisema Mengi.

Mengi ambaye pia ni mmiliki wa vituo vya televisheni vya ITV, EATV na Capital TV, alisema licha ya nchi za Afrika, Tanzania imekuwa ya kwanza kuzima mitambo ilhali wananchi hawakuwezeshwa kumudu gharama za ving’amuzi.

“Nchi ambazo zimeendelea kwa kila kitu kama Uingereza, Marekani, Japan na kwingineko kuzima mitambo ya analojia walitumia zaidi ya miaka minane kwa nini sisi tumewahi hivi wakati hatujajipanga?” alihoji Mengi.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Sahara Media Group na mmiliki wa Kituo cha Star Tv, Samwel Nyalla alisema hivi sasa wanaendesha biashara hiyo kwa hasara.

Nyalla alisema hadi mwaka 2015, hali itakuwa mbaya kutokana na kukosa ving’amuzi.
Mkurugenzi wa Utangazaji wa TCRA, Habby Gunze alisema wao hawakualikwa katika mkutano huo hivyo hawajui chochote. Gunze alimtaka mwandishi kwenda ofisini leo.

“Sisi hatujui chochote na kama unataka maelezo mengine njoo kesho (leo) ofisini kwetu uonane na Mkurugenzi Mkuu (Profesa John Nkoma), ili tuzungumze kwa ‘fact’ (kwa ushahidi) kipi kinachoendelea,” alisema Gunze.

Nukuu
Kama mamlaka itashindwa kurudisha ule mfumo wa analojia kuwa sambamba na dijitali hadi pale wananchi watakapokuwa na ving’amuzi tutazima televisheni zetu ndani ya mwezi mmoja ujao labda TBC ndiyo itakayobaki”.
Chanzo: Gazeti Mwananchi.

No comments:

Post a Comment