Friday, April 26, 2013

HATIMAYE BEI YA KIVUKO KITAKACHOTUMIKA KUTOKA BAGAMOYO MPAKA DAR YAJULIKANA NI TSH BIL 7.91.


Na Johary Kachwamba-Maelezo
UJENZI wa Kivuko chenye uwezo wa kusafiri kwa kasi ya kilometa 40 kwa saa moja, unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi nane kwa lengo la kupunguza msongamano wa magari jijini Dar-es-salaam.

Kivuko hicho kitakachotoa huduma ya usafiri kati ya Bagamoyo na Kigamboni kupitia Tegeta na vituo vigine sita (6), kina uwezo wa kubeba zaidi ya abiria 300.

Akizungumza jijini Dar-es-salaam wakati wa kusainiwa rasmi mkataba wa manunuzi ya kivuko hicho, Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli amesema pesa zote zilizotumika katika manunuzi ya kivuko hicho zimetolewa na Wakala wa Ufundi na Umeme (TAMESA) na hivyo ni pesa za wananchi.
"kupanda kwa nauli ya vivuko vyetu na usimamizi mzuri wa pesa zinazopatikana katika vivuko hivyo ndiyo matunda ya kupatikana kwa kivuko hiki, hakuna pesa ya msaada hapo ni pesa za watanzania" alisema Waziri Magufuli.
Mradi huu wa serikali umeanza na jiji la Dar-es-salaam na kuahidi kufanya hivyo hata kwa mikoa mingine inayoweza kutumia aina hii ya usafiri, kama Kigoma na Mwanza.
Aidha Serikali ameiasa kampuni yenye dhamana ya kujenga kivuko hicho kufuata makubaliano yaliyowekwa, kwa kukamilisha kazi hiyo kwa kiwango na wakati ili Watanzania wapate mbadala mwingine wa usafiri haraka.
kampuni ya M/S Johns Gram Hanssen kutoka nchini Denmark ndiyo iliyoshinda Zabuni ya ujenzi wa kivuko baada ya kuzishida kwa vigezo kampuni zingine 11 kutoka nchi mbalimbali, na gharama ya manunuzi ni dola za kimarekani dola 4,980,000/= sawa na Bilioni 7.91 shilingi za Tanzania.
Mwezi julai, 2012 TAMESA iliitisha mkutano wa Wadau kujadili jinsi ya kuweza kupunguza na kisha kumaliza kabisa msongamano wa magari jijini Dar-es-salaam, miongoni mwa wadau ni Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) na Mamlaka ya Bandari (TPA).
Moja ya mapendekezo ilikuwa ni ujenzi wa kivuko cha abiria kitakachotoa huduma kati ya Kigamboni na Bagamoyo, nasasa ununuzi wa kivuko hicho umekamilika, kwa usimamizi wa TAMESA ikushirikiana kwa karibu na Wizara ya Ujenzi.
Mkurugenzi wa TAMESA, Prof. Idrissa Mshoro amesema SUMATRA na TPA watawajibika kukagua Ubora wa kivuko mara kitakapo kamilika katika karakana ya West Marine, nchini Bagladesh, kwakuwa ujenzi wa kivuko hiki unafanyika nchini humo.
Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Johnny Flentø, amedhibitisha ubora wa huduma za kampuni yenye dhamana ya M/S Johns Gram Hanssen, huku akiridhia ujenzi kufanyikia Bangladesh kwakuwa watajenga haraka na kwa bei nafuu.
Kivuko hicho cha 23 kwa Tanzania, na chenye muundo wa kisasa zaidi kuweza kustahimili mabadiliko ya hali ya hewa, kitafungiwa vifaa vya kisasa vya mawasiliano na usalama.


MJENGWA BLOG

No comments:

Post a Comment