Thursday, September 6, 2012

CUF yamshambulia msajili wa vyama vya siasa John Tendwa.


George Kanuti
Mwenyekiti Cha Chama Wananchi(CUF), Ibrahimu Lipumba amemtuhumu Msajili wa Vyama Vya Siasa Nchini, John Tendwa kuwa anaendesha njama za kukizorotesha   chama chake na ametaka mamalaka za kiutendaji kuanzisha uchunguzi wa kimahesabu kwa ofisi ya msajili huyo.

Profesa Lipumba aliyekuwa akizungumza na Mwananchi alisema, chama chake kimeshangazwa na namna ofisi hiyo ya msajili ilivyotoa usajili wa kudumu kwa chama kipya cha kisiasa Democratic Change ADC ambacho kinadaiwa kuzoa wanachama wengi toka ndani ya CUF.

Kauli ya Profesa Lipumba inakuja siku chache baada ya ofisi ya msajili wa vyama vya siasa kutoa usajili wa kudumu kwa chama kipya ambacho wachunguzi wa mambo wanadai ni matokeo ya mvutano wa kiuongozi uliokikumba chama hicho na kusababisha baadhi ya wanasiasa ndani ya chama hicho kukitupa mkono na kuanzisha harakati mpya.

Kwa mujibu wa Profesa Lipumba, ofisi ya msajili wa vyama vya siasa inacheza karata yenye sura ya upendeleo ambayo pia imelenga kuzorotesha ngome ya vyama vya upinzani. “ Sisi tunashangaa msajili wa vyama kuwa na haraka ya kutoa usajili huu wa kudumu hivi alikuwa na haraka gani kufanya hivi?” alihoji Mwenyekiti huyo.

Alisema ofisi hiyo ya msajili, ilizuia kwa makusudi juhudi za kusajiliwa kwa chama kipya cha CCJ ambacho amedia kuwa kilikuwa na wafuasi toka chama tawala CCM lakini alichukua mkondo mwingine kutoa usajili wa kudumu kwa chama hiko kipya kwa vile waasisi wake ni kutoka chama cha CUF.
 “ Huyu msajili ana lake jambo, mbona wakati ule aliweka ngumu juhudi za kusajiliwa kwa chama cha CCJ? Au kwa vile waasisi wake walikuwa wakitoka ndani ya CCM, ... Sasa kwa vile wafuasi wa chama hiki wanatoka ndani ya Cuf basi haraka haraka ametoa usajili wa kudumu,”alisema Profesa Lipumba.

Mwenyekiti huyo ambaye chama chake kinakusudia kufanya mkutano mkubwa wa hadhara mwishoni mwa juma jijini Dar es Salaam, alisema kuna haja sasa ya kuanzisha uchunguzi wa kimahesabu dhidi ya ofisi ya msajili ili kufichua mambo yaliyojificha ndani yake.

“ Huyu msajili lazima sasa afanyiwe auditing, tujue anaendesha vipi mambo yake maana tunatilia shaka utendaji wake, haiwezekani chama kimoja leo kinakuja kuomba usajili  kinanyimwa kisha baadaye kinakuja kingine kinakubaliwa, lazima msajili huyu afanyiwe auditing,”alisisitiza Profesa Lipumba.

Alipotakiwa kuelezea mwelekeo wa chama chake kutokana na kumeguka kwa baadhi ya wanachama na viongozi wa kada ya kati waliojiunga na chama kipya cha ADC, Profesa Lipumba alisema “ hilo kwetu halitunyimi isingizi, isitoshe pia kila raia ana haki ya kuchagua na kujiunga na chama chochote akipendacho”.

Hata hivyo alisema, anashangazwa na tukio la mwanasiasa Hamad Rashid aliyetangaza kuwa mlezi wa chama hicho kipya cha siasa kwa kauli yake ya kukusudia kutumia uchaguzi mdogo wa Jimbo la Bububu visiwani Zanzibar kujipima namna kinavyokubalika kwa wapiga kura. 

“Huyu Hamad Rashid ,sisi tumemtimua kwenye chama, amekwenda mahakamani kupinga uamuzi wetu na sasa anatajwa kuwa mlezi wa chama kingine cha siasa, hivi kweli mtu anaweza kuwa mwanachama wa vyama viwili kwa wakati mmoja?” alihoji Profesa Lipumba na kuongeza kuwa:
 “ Kwa vile suala hili liko mahakamani tunaamini mahakama  inashuhudia mwenendo huu na itafanya kazi yake”.

Msajili wa vyama ajitetea 
Msajili wa vyama vya siasa John Tendwa amesema kuwa usajili wa chama hicho kipya haukuegemea matakwa ya upande fulani wa kisiasi bali ulifanyika kwa kuzingatia sheria na kanuni na wakati huo huo, amefungua milango kuwakaribisha wakaguzi wa mahesbu.

Alikosoa matamshi ya Profesa Lipumba aliyemtuhumu ofisi yake kukwamisha juhudi za usajili wa Chama Cha CCJ ambacho harakati zake ziligonga mwamba ikiwa imesalia miezi michache kabla ya kuanza mchaka mchaka wa kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2010 na hatimaye kuzaliwa kwa chama kingine cha CCK.

“Hiki Chama Cha CCJ ambacho Lipumba anakitolea mfano, hakikujipanga kilikuwa hakina wanachama, sasa mimi nitatoaje usajili kwa chama hakijatimiza masharti,”alisema Tendwa. 
Kwa mujibu wa Tendwa chama hicho hakikuchukua hatua zinazopaswa ikiwamo kutoa taarifa za uongo kuhusu wanachama wake na kukosa wawakilishi wa kutoka mikoani.

 “ Jambo la kushangaza hata baadhi ya viongozi wake hawakuwa wanachama. Mfano huyu Mpendazoe aliyehamia Chadema alikuwa ni Public Secretary wa chama, lakini hakuwa na kadi ya uanachama… ndugu yangu katika mazingira kama hayo chama kinawezaje kupata usajili wa kudumu”.
Kwa upande mwingine msajili huyo, alisema suala la utoaji usajili wa kudumu kwa chama chochote cha siasa linafanyika katika mazingira ya uwazi na ndivyo ilivyofanyika kwa chama kipya cha ADC ambacho alidai kuwa kilihitimisha masharti kwa wakati na hatimaye kukubalika kuanza rasmi shughuli za kisiasa.

Amemtaka Profesa Lipumba pamoja na wataalamu wengine kujitokeza katika ofisi yake kwa ajili ya kuendesha ukaguzi wa mahesabu na amesisitiza kuwa ofisi yake hufanyiwa ukaguzi wa mahesabu kila baada ya miezi mitatu.
Kupatiwa usajili wa kudumu kwa chama hicho kipya sasa kunafanya jumla ya vyama vya siasa ambavyo vimepata baraka ya kuendesha siasa kufikia 20. 

www.mwananchi.co.tz

No comments:

Post a Comment